Watu milioni 12 duniani kote hawana utaifa- UNHCR
Kampeni ya #I Belong au #Miminiwa, ikitimiza miaka minne mwezi huu wa Novemba, Kamishna Mkuu wa wakimbizi duniani, Filippo Grandi ametaka serikali zichukue hatua za haraka kuhakikisha ifikapo mwaka 2024 tatizo la watu kutokuwa na utaifa linatokomezwa
Filippo Grandi ambaye pia ni Mkuu wa shirika la kuhudumia wakimbizi duniani, UNHCR ametilia mkazo hoja hiyo wakati huu ambapo idadi ya watu ambao hawana utaifa kote duniani inakadiriwa kuwa milioni 12, ikielezwa kuwa athari za kukosa utaifa ni za papo kwa papo.
Bwana Grandi amesema kuchukua hatua haraka ni jambo muafaka kufanya kimaadili ,kiutu na kisiasa akiongeza kuwa watu wasio na utaifa bado wanakabiliwa na changamoto kupata haki zao za msingi kama vile elimu,matibabu, na ajira.
“Ondoeni sheria za kibaguzi ambazo ndio kichocheo cha ukosefu wa kitaifa,” amesema Grandi ikielezwa kuwa mataifa 25 duniani bado yana vipengele vya ubaguzi wa kijinsia ambavyo vinazuia watoto kupata uraia au utaifa wa mama zao kama ilivyo kwa upande wa baba.
Nchi zilizobadili sheria ni pamoja na Sierra Leone na Madagascar Kenya, Kyrgyzstan na Thailand nazo zikielekea kubadilisha sheria zake.
Miaka minne tangu uzinduzi wa kampeni ya miaka 10 ya #I Belong yenye lengo la kutokomeza ukosefu wa utaifa, zaidi ya watu 166,000 wamepatiwa utaifa.