ITU imechangia maendeleo ya TEHAMA Uganda
Uganda imepiga hatua kubwa katika sekta ya teknolojia ya habari na mawasiliano auTEHAMA ambapo hivi sasa asilimia 79 ya raia wake wanapata huduma za mawasiliano kupitia Broadband.
Akizungumza kwenye kongamano la Muungano wa kimataifa wa mawasiliano, ITU unaoendelea mjini Dubai katika Falme za kiarabu, waziri wa Uganda wa masuala ya TEHAMA na mwongozo wa kitaifa, Frank Tumwebaze, amesema kiwango hicho kimefikiwa wakati wananchi wengi wako sehemu za mashambani.Ameongeza kuwa taifa lake linatambua umuhimu wa kupiga hatua katika nyanja ya mawasiliano, ujumuishwaji, ushirikiano na ubunifu wa mwanadamu katika kufikia malengo ya maendeleo endelevu yaani SDG’s
“Tunathamini mchango wa ITU katika juhudi hizi.Tunaazimia kulinda hadhi ya ITU na pia kufanikisha malengo yake.Katika ngazi ya kitaifa Uganda imetambua maendeleo ya TEHAMA kama chombo muhimu cha kulisaidia taifa kuvuka hadikwenye kipato cha kati. Hivyo serikali ya Uganda imekuja na mpango wa kitaifa na sera kuhusu masuala ya kidigitali na broadband,na pia mwongozo wa kuziba pengo lililopo la kidigitali. Vilevile serikali imeunda mipango kadhaa ya TEHAMA mfano mfuko maalum la kuwasaidia vijana wabunifu.”
Waziri ameongeza kuwa aslimia 84 ya raia wake huishi vijijini na pia asilimia 54 ni vijana wenye umri usiozidi miaka 18 na mafanikio yaTEHAMA itakuwa mkombozi kwa watu hawa na taifa zima kwa ujumla.
Ameongeza kuwa kazi sasa iliobaki ni kupanua huduma hiyo kwa taifa zima na pia upatikanaji wake uwe wa gharama ndogo.