Msikate miti hovyo kwa kuwa jangwa lanyemelea Kenya -Mwanamazingira Masinde.
Ukataji holela wa miti kinyume na vibali ambavyo vinatolewa na serikali ni moja ya sababu za uharibifu wa mazingira nchini Kenya, amesema Isabella Masinde mtaalam wa mazingira, kutoka idara ya mazingira nchini humo.
Akihojiwa na Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa mjini New York, Marekani, Bi.Masinde,Mkurugenzi wa Mazingira na ulinzi wa masuala ya kijamii katika kamati ya kitaifa ya kupokea malalamiko kuhusu mazingira nchini Kenya amesema..
“Maendeleo yanaathiri mazingira wakati ..mambo ya kufanya mipango ya matumizi ya hayo mazingira hayatekelezwi, lakini kama kungekuwa na utaratibu wa kujua kama kwa mfano miti ikitolewa miti elfu moja tutaendelea vizuri. Lakini mtu anapewa leseni na anakwenda anakata miti karibu yote na hata ile michanga ambayo haistahili kukatwa kwa sababu Kenya ‘utaratibu’ ulioko ni kutoa leseni kwa wakata mbao nao wanakwenda wanakata kila kitu hawajali kama kuna ile inatakiwa iachwe..ama kuna ile inatakiwa ibakie ili kuendelea kuhifadhi mazingira kwa sababu ukikata sehemu kubwa, basi umesababisha mmomonyoko wa udongo.”
Hata hivyo amesema kwa sasa serikali inaweka mikakati mipya ya kuhakikisha kuwa kilaanayepatiwa kibali cha kukata miti anakata kwa mujibu wa kibali chake na kwamba maafisa wa mazingira wawepo ili kutathmini athari kwa mazingira.
Halikadhalika afisa huyo ametoa wito wa kulinda mazingira akisema .
“ Kila mtu ana jukumu la kulinda mazingira …kwa kupanda miti. Nchini Kenya kuna sheria inasema kila kaya, kila shamba nchi yote iwe na asilimia 10 ya eneo lake liwe na miti. Kama wewe shamba lako ni robo eka sasa utachukua asilimia 10 ya hiyo. Kama ni miti minne… kwa sababu sasa mnaona mafuriko yakitokea yanasomba mashamba na mazao yaliyopandwa kwa sababu hakuna kitu cha kushikilia. Mvua inataka ikinyesha maji yake yateremke polepole kwenye miti hadi yafike kwenye nyasi, msipofanya hivyo tutajikuta tuko jangwani.”