Watoto 9 kati ya 10 huvuta hewa chafu kila siku kote duniani: WHO
Zaidi ya asilimia 90 ya watoto duniani kote walio na umri wa chini ya miaka 15 huvuta hewa chafu kila siku ambayo inaweka maisha yao hatarini na wengi wao hufariki dunia imesema ripoti ya shirika la afya dunaini WHO.
Ripoti hiyo mpya ya WHO iliyotolewa leo mjini Geneva Uswisi, inasema kila siku watoto bilioni 1.8 walio katika umri wa chini ya miaka 15 wanavuta hewa chafu ikiwa ni sawa na asilimia 93 ya watoto wote , na WHO inakadiria kuwa mwaka wa 2016 pekee watoto 600,000 walifariki dunia kutokana mifumo yao ya kupumua kuathiriwa na hewa chafu.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt Tedros Adhanom Ghereyesus, hali hii haivumiliki kwani kila mtoto ana haki ya kuvuta hewa safi ili aweze kukua na kufikia uwezo wake katima maisha.
Ripoti hiyo kuhusu " uchafuzi wa hewa na afya ya mtoto" imezinduliwa katika mkesha wa mkutano wa kwanza kuhusu uchafuzi wa hewa na afya kuwahi kufanywa na WHO.
Mkurugenzi wa idara ya afya ya umma, mazingira na jamii wa shirika hilo , Dkt Maria Neira amesema hewa chafu inasababisha ubongo wa mtoto kudumaa na kuna njia nyingi za kusaidia kukabiliana na hewa hiyo chafuzi kwani
(SAUTI YA DKT MARIA NEIRA)
“ Wasiwasi wetu ni kuwa itasababisha madhara kwa mishipa ya fahamu na kufanya kiwango cha ufahamu wa mtoto kuwa chini katika kutambua mambo. lingine tunalojua ni kwamba uvutaji wa hewa chafu unauwezekano wa kusababisha ugonjwa wa pumu na ikiwa tayari unayo pumu basi hufanya hali kuwa mbaya zaidi.”
Amsema WHO inaunga mkono hatua za kisera kama vile kuharakisha hatua za kutumia nishati mbadala kwa ajili ya kupikia , usafiri usiochafua mazingira pamoja na nyumba zinazojali mazingira.
Ripoti imetaja athari nyingine za hewa chafu kwa mfano mama mjamzito akivuta hewa hiyo anaweza kujifungua mtoto kabla ya wakati au njiti na mtoto kuwa na uzito mdogo sana. Pia ripoti inaendelea kuainisha kuwa hewa chafu inaathiri neva na inaweza kusababisha ugonjwa wa pumu na saratani ya utotoni.
Vilevile watoto ambao wameathirika kwa kiasi kikubwa na hewa hiyo chafu wako hatarini kupata magonjwa kama vile ya moyo katika maisha yao ya baadae.