Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kiwango cha vifo vya mama wanaojifungua Sudan Kusini kiko juu : UNFPA

Mapigano nchini Sudan Kusini yameleta mkwamo kwa huduma za afya ya uzazi ikiwemo kwa wajawazito baada ya kujifungua. (Picha:UNMISS)

Kiwango cha vifo vya mama wanaojifungua Sudan Kusini kiko juu : UNFPA

Afya

Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia idadi ya watu la UNFPA limetoa wito wa kuchukuliwa hatua madhubuti za kukabiliana na tatizo la ghasia zilizo na uhusiano wa kingono pamoja na kijinsia nchini Sudan Kusini.

Wito huo umetolewa mjini Juba, mji mkuu wa Sudan Kusini , na mkunga wa UNFPA nchini humo, Bi Judith Draleru, katika mahojiano na Radio Miraya,  Radio ya Umoja wa Mataifa katika taifa hilo.Akisisitiza haja ya kuwapa matumaini waathirika  wa ubakaji ambao baadhi hupoteza maisha wakati wa kujifungua mimba ambazo hawakutarajia na pia  kugusia hali ilivyo nchini Sudan Kusini.

 “ Sisi kama UNFPA  mpango wetu wa kimkakati ni kuhakikisha kwamba  hakuna yeyote anaeachwa nyuma katika  kupata taarifana huduma kuhusu afya ya uzazi ikiwa ni pamoja na haki zao.Tunataka kufikia lengo hili katika kile tunachokiita ajenda ya mabadiliko. Kwanza tunalenga kumaliza vifo vya kina mama wakati wa kijifungua  na pili ni kukomesha ukatili  wa  kijinsia pamoja na ndoa za utotoni lakini pia  mila nyingine potovu.”

Pia amesema kuwa UNFPA inaendesha mradi wa kuimarisha huduma za ukunga Sudan Kusini ili kuona kwamba hakuna  anaeachwa nyuma kulingana na malengo ya maendeleo endelevu.

UNFPA imekuwa ikiwasaidia waathirika wa ghasia  za kingono na kijinsia nchini Sudan Kusini.