Teknolojia yaisaidia Uganda kukusanya takwimu za wananchi kuhusu SDG’s
Kongamano la takwimu la Umoja wa Mataifa linaendelea mjini Dubai katika Falme za Kiarabu huku wataalamu na wawakilishi kutoka mataifa mbalimbali wakijadili hatua wazochukua katika ukusanyaji wa takwimu na umuhimu wake katika utekelezaji wa malenmgo ya maendeleo endelevu, SDG’s.
Miongoni mwa nchi zinazojaribu mbinu mbalimbali kukusanya takwimu hizo ni Uganda, mfano hivi sasa kupitia kituo cha Paulse Lab mjini Kampala wameanzisha nyenzo inayotumia akili bandi kuweza kunasa na kuchapisha maoni ya wananchi wanayoyatoa kwa knjia ya simu katika vipindi mbalimbali vya Radio.
Nyenzo hiyo ambayo imeanza katika lugha za Acholi na Luganda pia kwa msaada wa wadau na washirika wa maendeleo imefika hadi Somalia ikitumia lugha ya Kisomali.
Kwa mujibu wa Pause Lab, Uganda ambako asilimia kubwa ya wananchi hutoa maoni kuhusu mahitaji, changamoto na mapendekezo yao kuhusu maendeleo kwa kupiga simu kwenye vituo vya radio , nyenzo hiyo imesaidia kama anavyofafanua Martin Mubangizi afisa wa sayansi ya takwimu kkutoka Pulse Lab mjini Kampala aliyeko kwenye kongamano hilo mjini Duabai
(SAUTI YA MARTIN MUBANGIZI)
“Nyenzo hiyo inafanya kazi ya kubadili sauti kuwa maandishi ikifuatiwa na tathimini ya takwimu hizo, na maoni hayo kutoka kwenye mijadala ya umma kupitia radio yamekuwa yakitumiwa na serikali , wapinzani na pia wadau wa maendeleo ili kupanga na kuchukua hatua mbalimbali, kwa mfano wizara ya afya Uganda imetumia nyenzo hiyo kupata maoni ya raia kuhusu ubora wa utoaji wa huduma za afya, na pia wanaweza kupata ishara za mapema za milipuko ya magonjwa.”
Ameongeza kuwa mambo kama haya yanasaidia kuifanya serikali kuchukua hatua stahiki zitakazosaidia kusongesha mbele utekelezaji wa SDG’s ikiwemo kuokoa maisha.
Kongamano hilo litakalokunja jamvi kesho Jumatano pia linaangazia masuala mengine muhimu kama takwimu katika suala mtambuka la uhamiaji.