Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hali katika Gaza ni tete, pande zote sitisheni ghasia: Mladenov

Kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu Mashariki ya Kati
UN Photo/Rick Bajornas)
Kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu Mashariki ya Kati

Hali katika Gaza ni tete, pande zote sitisheni ghasia: Mladenov

Amani na Usalama

Ghasia katika maeneo yanayokaliwa kwa nguvu na Israel kwenye ukingo wa magharibi wa mto Jordan ikiwemo Yerusalem Mashariki zinaongezeka huku mamlaka ya Israel ikiendelea na bomoabomoa na kuchukua kwa nguvu  nyumba za wapalestina.

Akihutubia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa hii leo kwa njia ya video, mratibu maalum wa umoja huo kwenye mchakato wa amani huko Mashariki  ya Kati Nickolay Mladenov amesema bomoa bomoa hiyo inayofanywa na Israel si halali hivyo ameiomba isitishe mara moja.

Akinukuu takwimu za ubomoaji zilizotolewana ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya kibinadamu, OCHA, Bwana Mladenov ameorodhesha nyumba zilizobomolewa.

 “Majengo 39 yalibomolewa au kuchukuliwa katika eneo la Ukingo wa Magharibi wa mto Jordan, yakiwemo majengo matano huko Yerusalem Mashariki ambako ghasia zinaongezeka na hivyo kuacha watu 33 bila ya makazi na pia kuathiri  maisha ya watu zaidi ya 100.”

Mratibu huyo amesema kuwa ghasia zinazohusiana na ulowezi zinaongezeka akisema kuwa mashambulio 23 yalifanywa na walowezi wa  Israel dhidi ya  wapalestina na hivyo kusababisha  kifo cha mtu mmoja  na kuwajeruhi wengine 12 pamoja na kuharibu mali.

Pamoja na kutaja vitendo vinavyofanywa na Israel, mratibu huyo maalum akaangazia pia vile vinavyotekelezwa kutoka upande wa wapalestina.

Mathalani amesema kuwa tarehe 7 mwezi huu mpalestina mmoja alishambulia na kuwaua kwa kuwapiga risasi raia wawili wa Isreal, akiwemo mwanamume mmoja na mwanamke, katika eneo la viwanda la Barkan kwenye Ukingo wa Magharibi wa mtoJordan ambapo mpalestina huyo alikimbia na hadi sasa anasakwa na vikosi vya vya usalama vya  Israel.

Halidhalika jana jumatano, wapalestina walivurumisha maroketi mawili kutoka Gaza hadi Israel ambayo nayo ilijibu mashambulizi kwa kurusha makombora 45 kuelekea upande wa palestina.

Bwana Mladenov amesema kwa ujumla hali ni tete ukanda wa Gaza  akikumbusha onyo la hivi karibuni la Benki ya Dunia kuhusu uchumi wa Gaza kuwa unaporomoka ambapo kiwango cha watu wasio na ajira ni asilimia 53 na zaidi ya asilimia 70  ni vijana. “Mtu mmoja kati ya wawili huko Gaza ni fukara,” amesema Mladenov.

Ametoa wito kwa Baraza la Usalama pamoja na marafiki wa Israel na Palestina kushirikiana na Umoja wa Mataifa kuzitaka pande zote kuacha hatua ambazo zitaweka  hali ambayo italeta madhila kwa wengine wasio na hatia.

Pia amezitaka pande zote  kuendelea na makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyoridhiwa mwaka 2014.

Ameyataka makundi yenye silaha kama vile Hamas na mengine kuachana na uchokozi, na mashambuliio ya maroketi na visa vyote vya kiuchokozi dhidi ya Israel.

Na kwa Israel, Mladenov, ameitaka irejeshe huduma za upelekaji wa bidhaa muhimu hadi Gaza na pia  kuboresha njia za kusafirishia bidhaa na kwa  watu.