Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Utu na ubinadamu wafaa kurejea tunapojadili wakimbizi: Türk

Wafanyakazi wa UNHCR wakikitoa msaada kwa wakimbizi na waomba hifadhi baada ya mapigano kuibuka tena nchini Libya.
UNHCR/Sufyan Ararah
Wafanyakazi wa UNHCR wakikitoa msaada kwa wakimbizi na waomba hifadhi baada ya mapigano kuibuka tena nchini Libya.

Utu na ubinadamu wafaa kurejea tunapojadili wakimbizi: Türk

Amani na Usalama

Umewadia wakati wa kurejesha na kuzingatia utu na ubinadamu tunapohusika na mjadala mkali unaoendelea kuhusu masuala ya wakimbizi. Ni wito uliotolewa na kamishina msaidizi wa ulinzi wa kimataifa katika shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR.

Katika hotuba yake leo mjini Geneva Uswis  kwenye jukjwaa la kila mwaka la kamati tendaji ya UNHCR mkuu huyo, Volker Türk, amezungumzia kuhusu uhamasishaji wa majadiliano ya umma kuhusu suala la wakimbizi na kusema majadiliano hayo yana pande mbili .

 

Rohingya wavuka mto Naf ili kufikia kambi za wakimbizi nchini Bangladesh
© UNHCR / Andrew McConnell
Rohingya wavuka mto Naf ili kufikia kambi za wakimbizi nchini Bangladesh

Katika upande mmoja amesema kuna nuru iliyowahamasisha nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa 193 kuunda mkataba wa kimataifa kuhusu wakimbizi na kudhihirisha nini kinachoweza kufikiwa watu wanapoamua kuangalia suluhu ya muda mfupi na kuwa na lengo la pamoja. Ametolea mfano walioamua kukumbatia wakimbizi akisema

(SAUTI YA VOLKER TURK)

“Hususan katika bara la Afrika tumeshuhudia makundi ya wachache ambao awali hawakuwa na uraia  wakipewa uraia na vitambulisho, jinsi gani wanawake wakimbizi wa ndani walivyoweza kujimudu tena na kuanza maisha mapya.”

 

Wakimbizi wa ndani jimbo la Darfur Sudan wanakabiliwa na changamoto nyingi na ugumu wa kupata maji safi. Pichani ni msichana na kaka yake wakiwa katika kituo cha maji safi cha Abu-Shok kwenye kambi ya wakimbizi wa ndani illi kuteka maji
UNAMID/Mohamad Mahady
Wakimbizi wa ndani jimbo la Darfur Sudan wanakabiliwa na changamoto nyingi na ugumu wa kupata maji safi. Pichani ni msichana na kaka yake wakiwa katika kituo cha maji safi cha Abu-Shok kwenye kambi ya wakimbizi wa ndani illi kuteka maji

Na katika upande mwingine wa shilingi Bwana Turk ameongelea juu ya matokeo ya mataifa kutumbukia katika shinikizo na kuacha kutekeleza majukumu yao na kuongeza

(SAUTI YA VOLKER TURK)

“kwa mfano watoto walipokuwa wakigonga vichwa ukutani kwa kukata tamaa baada ya kutenganishwa na wazazi wao, au wakati vijana wadogo waomba hifadhi walipojiua baada ya kushikiliwa na kunyanyaswa kwenye vituo vya uandikishaji bila kuwa na matumaini yoyote ya mustakabali wao, au wakati raia waliokimbia na kujikuta wamekwama mpakani na kunyimwa vibali vya kuingia.”

 

Amesisitiza kuwa dunia hivi sasa inakabiliwa na mmomonyoko wa kutoheshimu utu wa binadamu hasa ukizingatia kwamba vita na mateso vimewafungisha virago watu milioni 68.5 duniani na miongoni mwao milioni 25.4 ni wakimbizi.