Watu milioni 1.4 kupewa chanjo dhidi ya kipindupindu Harare: WHO
Serikali ya Zimbabwe pamoja na wadau wake likiwemo shirika la afya duniani WHO leo wamezindua kampeni ya chanjo dhidi ya ugonjwa wa kipindupindu, OCV inayolenga watu milioni 1.4 kwenye mji mkuu Harare.
Taarifa ya WHO iliyotolewa leo mjini Harare inasema kampeni hiyo ya chanjo ni sehemu ya juhudi za kudhibiti mlipuko wa kipindupindu ulioripotiwa tarehe 6 mwezi uliopita wa Septemba na kwamba chanjo hiyo imetolewa na ubia wa chanjo duniani, GAVI, ubia ambao pia unagharimia kampeni nzima.
Mkurugenzi wa WHO kanda ya Afrika, Dkt Matshidiso Moeti, amesema kuwa mlipuko wa sasaumejikita zaidi katika viunga vya Harare ambako kuna idadi kubwa ya watu, lakini kuna fursa ya kukabiliana nao kupitia chanjo hiyo ili kuepuka ugonjwa huo kuenea zaidi kwenye maeneo mengine ambako itakuwa vigumu kuudhibiti.
Mbali na chanjo , serikali ikisaidiwa na WHO imeweka mikakati mingine ya udhibiti kama vile utoaji wa maji safi, na kuhimiza usafi, kusafisha mitaro ya na pia kuweka vituo kadhaa vya matibabu.
Chanjo dhidi ya kipindupindu itakuwa ya awamu mbili ikitilia mkazo mitaa ya Harare na Chitungwiza ulioko umbali wa kilomira 30 kusini mashariki mwa mji mkuu ambayo iliathirika mno na mlipuko huu .
WHO inasema ili kuepusha usugu wa muda mrefu kwa wananchi, dozi ya pili itatolewa katika maeneo yote wakati wa duru ya pili ya chanjo hapo baadaye.
Afisa Mtendaji Mkuu wa GAVI Dkt Seth Berkley, amesema kuwa kipindupindu ni ugonjwa ambao unaweza kuzuilika kwa kutumia maji safi pamoja na kuzingatia usafi na kuongeza kuwa hakuna sababu kwanini watu wawe wanaendelea kufa kutokana na ugonjwa huu mbaya.
Pia amesema kuwa GAVI imefanya juhudi kubwa kuona kama dawa ya chanjo dhidi ya kipindupindu huwa iko tayari wakati wowote ili kusaidia kukabilina na milipuko kama huo.
Kipindupindu kimekuwa kikitokea kila mara nchini Zimbabwe ambapo mlipuko mkubwa ulitokea Agosti 2008 hadi Mei 2009 na kuwaua watu zaidi ya 4000.