Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Tuimarishe ushirikiano wa kimataifa ili kunusuru uhamiaji- Grandi

Wafanyakazi wa UNHCR wakikitoa msaada kwa wakimbizi na waomba hifadhi baada ya mapigano kuibuka tena nchini Libya.
UNHCR/Sufyan Ararah
Wafanyakazi wa UNHCR wakikitoa msaada kwa wakimbizi na waomba hifadhi baada ya mapigano kuibuka tena nchini Libya.

Tuimarishe ushirikiano wa kimataifa ili kunusuru uhamiaji- Grandi

Wahamiaji na Wakimbizi

Kamishna mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR Filippo Grandi ametoa wito kwa mataifa kushirikiana ili kupata ufumbuzi wa suala la wakimbizi akisema makubaliano mapya  kuhusu wakimbizi  yatageuza hifadhi kuwa jibu mujarabu.

Kamishna Mkuu Grandi, amesema hayo leo  mjini Geneva Uswisi, wakati akifungua mkutano wa 69 wa mwaka wa Kamati tendaji ya UNHCR.

Ametaka kuimarisha zaidi  ushirikiano wa kimataifa ili kuweza kukabiliana vilivyo na ongezeko la migogoro   inayozidi kupanuka ambayo amesema imewalazimisha watu wengi kuhama makazi yao katika sehemu nyingi duniani.

“Misingi ya ushirikiano wa kimataifa imepata shinikizo kubwa, lakini licha ya hayo ushirika bado umesimama kidete. Lakini ni lazima tuongeze nguvu,” amesema Bwana Grandi akiongeza kuwa tangu achukue hatamu za shirika hilo, mwaka wa 2016, migogoro ya ndani imeongezeka ikichochewa na uhasama wa kikanda na wa kimataifa, na kuongezewa chumvi na  umaskini, ubaguzi wa rangi pamoja na mabadiliko ya tabianchi.

Ikiwa hiyo haitoshi amesema kuwa nazo kauli za kisiasa zimekuwa kali na kutoa mwanya kwa ubaguzi wa rangi na chuki dhidi ya wageni.

Grandi akiita tukio muhimu katika ushirikiano  mkubwa, amesema kuwa tamko la New York la mwaka wa 2016 kuhusu wakimbizi na wahamiaji, lilidhihirisha  azma ya kisiasa ya hali ya juu ambayo inahusu  ushirikiano wa kimataifa  pamoja na viwango vya kuwalinda wakimbizi.

Pia amekaribisha makubaliano mapya kuhusu uhamiaji ambao utapitishwa baadaye na Baraza Kuu la Umoja waMataifa akisema ni njia mpya na ya wazi ya kuchukua  hatua bora.

Ameongeza kuwa, “naamini ni uthabiti wa ushirikiano wa kimataifa- kama ushahidi dhahiri dhidi ya kauli  za kichochezi ambazo zinashamiri kwenye majukwaa kuhusu wakimbizi na wahamiaji.”

Akigusia muhula wake jinsi ulivyokuwa Grandi amebaini kuwa migogoro kama ile ya  Syria, Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo-DRC, na Kaskazini mwa Amerika Kusini imeendelea huku mingine kama vile Yemen, imezidi kupanuka.

Ametaja baadhi ya migogoro kama ile ya Iraq, kanda ya ziwa Chad na Sudan Kusini kama inayoelekea katika hali ya utulivu lakini bila ya ufumbuzi kamili.

Hotuba ya Grandi katika mkutano wa 69 wa kamati kuu inakuja wakati idadi ya waliofurushwa makwao ikiongezeka na kufikia watu milioni 68.5 ambapo watu milioni 25. 4 kati yao wamesaka hifadhi nchi za ugenini ilhali milioni 40 ni wakimbizi wa ndani.

Ameongeza kuwa maelfu kadhaa  wanaendelea kuvuka eneo la Sahel na baharí ya Mediteranea kuelekea Ulaya ambao wamekatishwa tamaa na kukabiliwa na ukatili pamoja na hatari zingine.

Grandi ameomba kuwepo na moyo wa kutoa hifadhi barani Ulaya  akisema , kile kilichopewa jina la uokozi baharini kimetekwa na siasa.