Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mkataba dhidi ya tumbaku umeboresha afya ya umma- WHO

Mwanaume akivuta sigara katika eneo lililotengwa kwa ajili ya wavuta sigara kwenye Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York Marekani.
UN News/Yasmina Guerda
Mwanaume akivuta sigara katika eneo lililotengwa kwa ajili ya wavuta sigara kwenye Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York Marekani.

Mkataba dhidi ya tumbaku umeboresha afya ya umma- WHO

Afya

Mkurugenzi Mkuu wa shirika la afya duniani WHO, Dkt Tedros Adhonom Ghebreyesus ameusifu mkataba  wa kimataifa wa kudhibiti matumizi ya tumbaku, FCTC, kama moja ya mafanikio makubwa ya afya kwa jamii katika kipindi cha  miaka 20 iliyopita.

Dkt. Tedros amesema hayo leo mjini Geneva Uswisi kabla ya kuanza kwa  mkutano  wa nane nchi wanachama wa mkataba huo, (COP8) , mkutano wenye lengo la kuanisha mwelekeo wa kuimarisha na kupanua wigo wa mkataba huo wa aina yake duniani.

Dkt Tedros amesema kuwa tangu mkataba huo uanze kutumika miaka 13 iliyopita,  umesalia kuwa nyaraka muhimu inayotumiwa duniani kuendeleza afya ya jamii.

Amesema kupitia mkataba huo nchi nyingi zimepitisha  sheria za kudhibiti matumizi ya tumbaku ikiwemo kuongeza kodi kwa bidhaa za tumbaku, kuweka maeneo salama ambako hairuhusiwi kuvuta sigara na kutaka kuwekwa kwa onyo lenye maandishi makubwa  katika bidhaa za tumbaku, mfano sigara.

Katika mkutano huu wa COP8 ambao  unajumuisha wajumbe  kutoka mataifa 137 wakiwemo wajumbe kutoka mashirika kadhaa ya Umoja wa Mataifa, kutazinduliwa ripoti mpya, iliyopewa jina la ,  “Ripoti ya WHO kuhusu maendeleo ya utekelezaji wa FCTC duniani,” ambayo inamulika ripoti mbalimbali  ambazo ziliwasilishwa na wahusika wa mkataba huo  katika kipindi cha mwaka wa 2018.

Mwanaume akivuta sigara pembezoni mwa barabara katika eneo la vijijini Nepal.
World Bank/Aisha Faquir
Mwanaume akivuta sigara pembezoni mwa barabara katika eneo la vijijini Nepal.

Ripoti inamulika  mafanikio duniani ya kudhibiti matumizi ya tumbaku kutoka katika hatua za kudhibiti na utekelezaji ambao utawezesha kupunguza matumizi ya tumbaku, pamoja na changamoto zilizopo kutokana na mapengo katika será na viwanda vya sigara.

Kikubwa kitakachojadiliwa katika mkutano wa COP8, unaoanza leo hadi tarehe sita Oktoba, ni kuweka mkakati jaribio wa kipindi cha kadiri ambao utaeleza  vipaumbele vya kuongeza na kuimarisha ajenda ya kudhibiti tumbaku ulimwenguni na pia kuimarisha utekelezaji wa mkataba hadi kipindi kingine cha miaka mitano.

Hii inahusu miongoni mwa mengine kuona kama juhudi za kudhibiti tumbaku zinahusu pia  mwelekeo mpya  kuhusu madhara ya bidhaa za tumbaku dhidi ya maendeleo na mazingira.

Mkurugenzi Mkuu wa ofisi ya Umoja wa Mataifa mjini Geneva, Michael Moller, amekariri umuhimu wa kuunganisha  udhibiti wa tumbaku na mikakati ya malengo ya maendeleo endelevu akimaanisha kulenga asilimia 80 ya wavutaji sigara duniani bilioni 1.1 ambao huishi katika mataifa yenye kipato cha chini na cha wastani.