Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mashambulizi dhidi ya raia yaongezeka Beni: UNHCR

Askari wa kikosi cha FIB akishika doaria  Beni Mashariki mwa DRC ambapo UN ilikuwa inasaidia jeshi la serikali katika operesheni zake.
Photo: MONUSCO/Sylvain Liechti
Askari wa kikosi cha FIB akishika doaria Beni Mashariki mwa DRC ambapo UN ilikuwa inasaidia jeshi la serikali katika operesheni zake.

Mashambulizi dhidi ya raia yaongezeka Beni: UNHCR

Wahamiaji na Wakimbizi

Shirika la kuhudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa, UNHCR limesema lina wasiwasi kuhusu usalama wa maelfu ya raia katika eneo la Kaskazini Mashariki mwa Jamhuri ya kidemokrasi ya Congo, DRC ambako ghasia za makundi yenye silaha zimeongezeka na za hivi karibuni zimesababisha vifo vya watu zaidi ya 20. Taarifa zaidi na Assumpta Massoi.

Wasiwasi huo wa UNHCR umeelezwa leo na  msemaji wa shirika hilo, huko Geneva, Uswisi, Babar Baloch wakati akizungumza na waandishi habari kuelezea hali ilivyo wakati huu ambapo kuna kampeni ya kutokomeza mlipuko wa Ebola.

Bwana Baloch amesema mashambulio yanaongezeka  katika mji wa Beni ulioko jimbo la Kivu Kaskazini pamoja na  jimbo la Ituri, maeneo ambayo yako mpakani mwa DRC na Uganda.

Amesema mwishoni mwa wiki kundi la ADF- NALU lilishambulia Beni na kuua watu zaidi ya 20 wengi wao raia na kwamba , "“Hii ni mara ya kwanza mapigano kufika katika mji wa Beni.  Na katika shambulio lingine katika mji wa Oicha, karibu na Beni kundi  lililojihami ambalo linashukiwa kuwa la ADF-Nalu, lilimuua kwa kumpiga risasi, mtu mmoja mwenye umri wa miaka 47 na kuteka takribani watoto wanane,  walipora mali na kisha  kuzichoma  moto nyumba kadhaa .”

Kwa mantiki hiyo amesema UNHCR inatoa wito kwa wanaohusika katika mgogoro huo kuheshimu na kulinda maisha ya watu waliopoteza makazi yao katika eneo hilo ambalo tayari linakabiliwa na mlipuko wa Ebola.

Walinda amani kutoka Malawi walio katika kikosi maalum cha kujibu mashambulizi cha ujumbe wa Umoja wa Mataifa huko DRC, MONUSCO wakiwa doriani huko Oicha na Erengeti mjini Beni, Kivu Kaskazini.
MONUSCO/Anne Herrmann
Walinda amani kutoka Malawi walio katika kikosi maalum cha kujibu mashambulizi cha ujumbe wa Umoja wa Mataifa huko DRC, MONUSCO wakiwa doriani huko Oicha na Erengeti mjini Beni, Kivu Kaskazini.

Kuhusu watu wanaovuka mpaka hadi Uganda wakikimbia ghasia kutoka DRC, UNHCR inasema kuwa idadi bado ni ile ile ambapo kwa wastani kwa siku wakimbizi 200  huingia Uganda na kwa mwezi ni 600.

Hata hivyo amesema, “Kuwasili kwa wakimbizi ni sehemu ndogo tu ya mwelekeo wa kila siku wa watu wanaovuka mpaka wa DRC na Uganda kwa sababu zingine kama vile biashara au kutembelea jamaa na marafiki na masuala mengine.”

 Amesema ili kuepusha kuenea kwa Ebola, UNHCR inachangia juhudi za shirika la afya duniani WHO  pamoja na serikali ya Uganda  kuwapima watu wanaovuka mpaka hadi Uganda  na imeweka vituo kadhaa  vya kuwapimia kiafya wakimbizi na hadi sasa hakuna kisa chochote cha Ebola kilichoripotiwa kutoka kwa wakimbizi.