Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Israel yadai imebaini bohari la siri la silaha za atomiki nchini Iran

Waziri Mkuu wa Isreal, Benjamin Netanyahu akihutubia mkutano wa 73 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.
UN Photo/Cia Pak
Waziri Mkuu wa Isreal, Benjamin Netanyahu akihutubia mkutano wa 73 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.

Israel yadai imebaini bohari la siri la silaha za atomiki nchini Iran

Amani na Usalama

Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu amehutubia mjadala mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mjini New York, Marekani huku akijinasibu kuwa wamebaini bohari la kisiri la silaha za atomiki nchini Iran lenye tani 300 za vifaa vya nyuklia.

Waziri Mkuu wa Israel akiwa amesimama katika mimbari ya ukumbi wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, ameonyesha picha  ya kile anachodai ni pahali ambapo pamefichwa vifaa vya nyuklia  huko Tehran, mji mkuu wa Iran.

Amedai kuwa “mwezi Mei tulifichua eneo kulikohifadhiwa mabaki ya siri ya mpango wa atomiki.Iko hapa. Katika kitongoji cha Shorabad cha mji wa Tehran. Leo nafichua eneo la pili la ghala la siri la atomiki ya Iran. Iko hapa, katika  mtaa wa Turouzabad mjini tehran, umbali wa maili sita.”

Vile vile  ameonyesha  maeneo ambako anadai kuwa kumefichwa kile alichosema ni makombora ya Hezbollah  karibu na uwanja wa ndege wa kimatifa wa Beirut nchini Lebanon.

Waziri Mkuu huyo wa Israel amesema “Hezbollah kimakusudi wanatumia raia wa Lebanon wasio na hatia , kama ngao. Wameweka makombora katika maeneo matatu karibu na uwanja wa ndege wa kimataifa wa Beirut .”

Baadaye akaonyesha picha ya sehemu anayosema kumefichwa makombora hayo.