Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hatutakubali tena upatanishi wa Marekani pekee- Rais Abbas

Rais wa Palestina, Mahmoud Abbas wakati akihutubia mjadala mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, kikao cha 73
UN/Cia Pak
Rais wa Palestina, Mahmoud Abbas wakati akihutubia mjadala mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, kikao cha 73

Hatutakubali tena upatanishi wa Marekani pekee- Rais Abbas

Amani na Usalama

Wapalestina pamoja na eneo lao hivi sasa wanahitaji zaidi ulinzi wa haraka kutoka kwa jamii ya  kimataifa kuliko wakati wowote ule.

Ombi hilo limetolewa leo  na Rais wa Palestina, Mahmood Abbas, mjini New York, Marekani wakati akihutubia mjadala mkuu wa mkutano wa 73 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.

Rais Abbas ameomba jamii ya kimataifa   kutafuta mbinu za kuwapatia wapalestina ulinzi wa  haraka iwezekanavyo,  kufuatia  hatua ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa  ya  tarehe 13 mwezi Juni mwaka huu ya kupitisha azimio kuhusu kuwalinda  raia wa taifa hilo.

Amesema ingawa  wanakaribisha  msaada wa kiuchumi na wa kibinadamu kwa eneo la  ukingo wa magharibi wa mto Jordan na ukanda wa Gaza, kupitia taasisi alizoita , “halali za Palestina”, kamwe hawatakubali msaada huo kuwa ndio suluhisho la kisiasa ambalo litamaliza  hatua ya Israel , aliyosema ya  “kukalia ardhi yao”  na pia kuwapatia uhuru .

Ameongeza kuwa msaada huo pia hauwezi kuchukua pahala pa kuondoa mzingiro wa Israel na pia kukomesha  mgawanyiko kati ya Gaza  na ukingo wa magharibi na kusema kuwa kamwe hawatetereka kupinga hatua za kutenga  Gaza kutoka kwa taifa la Palestina.

Kuhusu suala la upatanishi, Rais huyo wa wapalestina, amesema kuwa hawatakubali  usuluhishi wa Marekani pekee katika mchakato wa kuleta amani akisema ni kwa sababu  utawala wa Marekani umepoteza uhalali katika mgogoro huo wa mashariki ya kati kutokana na matukio ya hivi karibuni.

Mbali na Marekani kutambua Yerusalem kama mji mkuu wa  taifa la Israel na kuhamisha ubalozi wake kutoka Tel Aviv hadi Yerusalam pia utawala wa Marekani ulifuta ufadhili kwa shirika la Umoja wa mataifa linalosaidia wakimbizi wa kipalestina.