Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uhamiaji yafaa uwe salama na wa mpangalio: Guterres

Wahamiaji wakiwa kando mwa bahari mjini Lesbos, Ugiriki.
IOM/Amanda Nero
Wahamiaji wakiwa kando mwa bahari mjini Lesbos, Ugiriki.

Uhamiaji yafaa uwe salama na wa mpangalio: Guterres

Wahamiaji na Wakimbizi

Serikali, asasi za kiraia pamoja na mamlaka za kikanda  zimehimizwa kujitayarisha vyema  kwa mkutano mkuu kuhusu uhamiaji zikiwa tayari kuweka azma kuwa zitatumia  faida za uhamiaji uliosimamiwa vizuri kwa minajili ya  kupunguza  athari mbaya za sera mbovu na kutokuwepo ushirikiano katika suala zima la uhamiaji.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa , Antonio Guterres, amesema hayo leo katika hotuba yake kwenye mkutano wa ngazi ya juu kuhus uhamiaji jijini New York, Marekani, mkutano uliopatiwa jina “mwelekeo hadi Marrakesh,” ambako kutafanyika mkutano wa kimataifa wa uhamiaji.

Bwana Guterres amesema mkataba wa kimataifa kuhusu uhamiaji utarahisisha uhamiaji wa aina yote  ili uwe, “ salama , wenye mpangilio na  wenye kuondoa adha.”

Amesema kuwa  suala la uhamiaji linamhusu kila mtu na kuongeza  kuwa, athari zake  za kiuchumi zinagusa hata kampuni na mashirika  makubwa ya kimataifa.

Akiendelea kuumwagia sifa mpango mpya kuhusu uhamiaji , Bw Guterres akisema unatilia mkazo haja ya  ushirikiano katika juhudi za kushughulikia suala hilo na kuongeza kuwa unatambua  kuwa mbali na  kila taifa  linawajibika na kile kilichoko ndani ya mpaka wake, lakini duniani hii ya kutegemeana  inahitaji ufumbuzi ulioegemea ushirikiano na kufuata yale ambayo yanafanana.

 

Wahamiaji wakivuka mto kimagendo karibu na Cucuta katika  mpaka kati ya Colombia-Venezuela. Ni 'kivuko' muhimu kwa wahamiaji haramu.
WFP/Jonathan Dumont
Wahamiaji wakivuka mto kimagendo karibu na Cucuta katika mpaka kati ya Colombia-Venezuela. Ni 'kivuko' muhimu kwa wahamiaji haramu.

Katibu Mkuu amesema ameanzisha  mtandao mpya wa uhamiaji ndani mwa Umoja wa Mataifa ili kuunga mkono mataifa  wanachama katika utekelezaji  wa mkataba wa uhamiaji akisema mkataba huo utasaidiwa kwa karibu na shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji IOM.

Kwa sasa inakadiriwa kuwa  kuna wahamiaji milioni 260 duniani ambapo nusu yao ni wanawake na wasichana ambapo Guterres amesema, “utekelezaji wa  mkataba wa uhamiaji unapaswa kusikiliza sauti na mahitaij yao.”

Naye rais wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, Bi. María Fernanda Espinosa, amesema kuwa, wakati huu suala la uhamiaji limeigawanya dunia kutokana na athari zake kisiasa, kijamii na  kiuchumi.

Ameongeza kuwa ingawa hawawezi kurudisha  nyuma yaliyopita, amesema ni wakati wa kuganga yajayo na kusema wanaweza kubadili ya hapo baadaye.

Amesema kuwa ni muhimu kwa jamii ya kimataifa kupiga tochi katika hali ya usoni na kutafakari jinsi ya  kulishughulikia na kusema kuwa kwa kufanya hivyo ni sharti kuzingatia kuwa  ingawa uhamiaji hutoa  nafasi sawa  kwa wahamiaji na wenyeji, lakini wale wanaopinga  uhamiaji huenda hutizama tu changamoto za ukweli au za kudhaniwa.