Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

"Tunaushukuru Umoja wa Mataifa kwa kujadili moja ya matatizo yetu makubwa": Tanzania

Mhudumu wa afya akiwapatia ushauri nasaha wanawake kuhusu matibabu dhidi ya Virusi Vya UKIMWI, VVU na UKIMWI
UN/maktaba
Mhudumu wa afya akiwapatia ushauri nasaha wanawake kuhusu matibabu dhidi ya Virusi Vya UKIMWI, VVU na UKIMWI

"Tunaushukuru Umoja wa Mataifa kwa kujadili moja ya matatizo yetu makubwa": Tanzania

Afya

Mjadala wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kikao cha 73 unaendelea  mjini New York Marekani na leo , unajikita katika afya hususan  jinsi ya kupambana na ugonjwa wa kifua  au TB kikuu kote duniani.

Shirika la afya ulimwenguni WHO, wataalamu wa afya, watafiti na mawaziri wa afya  na wawakilishi wa sekta za afya kutoka nchi wanachama wanahudhuria mjadala huo.  Tanzania  inawakilishwa na Ummy Mwalimu ambaye ni waziri wa afya, maendeleo ya jamii, jinsia watoto na wazee.

Akizungumza na Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa amesema moja ya mambo yaliyoifurahisha Tanzania katika mjadala wa Baraza Kuu mwaka huu ni kuamua kujadili Ugonjwa wa kifua kikuu.

“Tunashukuru kuona umoja wa mataifa unajadili ugonjwa wa kifua kikuu kwasababu Tanzania ni moja ya nchi 30 zenye idadi kubwa ya wagonjwa wa kifua kikuu”

Ni Waziri wa Afya nchini Tanzania akieleza hali ya Ugonjwa wa kifua kikuu ilivyo nchini mwake.

Waziri Ummy, pia anasema pamoja na Tanzania kujitahidi katika matibabu, changamoto kubwa ambayo nchi yake Bado inakabiliana nayo ni kuwaibua wagonjwa wapya wa Kifua kikuu. Amesema inakadiriwa kuwa katika watu 100 wenye Ugonjwa wa kifua kikuu nchini Tanzania, 56 kati yao hawajafikiwa ili kuingizwa katika utaratibu wa matibabu.

Je! Wana wana mkakati gani kuwatambua wagonjwa wapya na kuwafikishia matibabu?

“Sasa hivi, mtu yeyote ambaye ataenda katika kituo cha kupata huduma za afya tutamuhisi kama mgonjwa wa kifua kikuu. Kwa hiyo ataulizwa vidokezo kama kumi hivi ambavyo vitatusaidia kumweka kwenye nafasi ya pili.”

Amesema tiba za jadi ni changamoto wanakabiliana nayo kwa kutoa elimu

 “Tumewapa mafunzo waganga wa kienyeji na tumewaeleza pale ambapo mtu amekuja kwako ana kifua kikuu umempa dawa zako, siku ya kwanza ya pili hapati nafuu yoyote, mpe rufaa”

Aidha Tanzania kwa kushirikiana na wakfu wa kimataifa wa kupambana na Ukimwi, Malaria na Kifua Kikuu Global Fund, wamenunua mashine mpya za kupima ambazo hutoa majibu ndani ya muda mfupi wa saa mbili.

Ripoti ya  shirika la afya ulimwenguni WHO iliyotolewa katikati ya mwezi huu kuhusu hali ya ugonjwa wa  TB duniani, inasema  idadi ya watu waliougua kifua kikuu au kufariki dunia mwaka jana  ilikuwa ni ndogo ingawa bado mataifa mengi hayachukui  hatua za kutosha kuweza kutokomeza ugonjwa huo  ifikapo mwaka wa 2030.

Ripoti hiyo imeongeza kuwa licha ya  juhudi zilizoweza kuzuia vifo vya watu milioni 54  duniani kote kutokana na kifua kikuu tangu mwaka wa 2000, bado  TB inasalia kuwa ugonjwa hatari wa kuambukiza.