Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNICEF yazindua mpango wa kuinua mtindo wa usafi shuleni, Uganda

Uhaba wa maji nchini Sudan Kusini siyo tu ni tishio kwa amani na usalama bali pia maendeleo kwa kuwa wananchi wanatumia maji yasiyo safi na salama na kupata magonjwa. (Picha:Unifeed video)

UNICEF yazindua mpango wa kuinua mtindo wa usafi shuleni, Uganda

Afya

Shirika la Umoja wa  Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF kwa msaada kutoka kwa serikali ya Korea Kusini limezindua mradi unaolenga kuhakikisha upatikanaji wa maji safi na huduma za kujisafi katika shule zaidi ya 100 nchini humo. 

Mradi huo umezinduliwa leo kwenye shule ya msingi ya Matany katika wilaya ya Napak, kaskazini Mashariki mwa Uganda  ukilenga kutekelezwa katika wilaya nane za eno la Karamoja ambako upatikanaji wa maji ni changamoto kubwa.

UNICEF imezundia mradi huu kwa msaada kutoka kwa shirika la ushirikiano wa kimataifa la serikali ya Korea Kusini (KOICA).

Mradi huu utahakikisha kwamba shule zote katika eno la Karamoja zimepata vifaa vya kuosha mikono ili kuinua “mitindo ya kuosha shuleni” ifikapo mwaka 2023.

Watoto 56,000 katika shule 100 ndio watanufaika moja kwa moja  na mradi huu wakifikia maji safi na kuduma za kujisafi.

Mwakilishi wa UNICEF Uganda, Dkt Doreen Mulenga anatumai kuwa mradi huu utaboresha mazingira ya elimu na afya shuleni kwa kupunguza hatari ya magonjwa yatokanayo na uchafu.

Akitoa mfano wa ugonjwa wa kuhara, Dkt Mulenga amesema kuosha mikono kwa kutumia sabuni kunaweza kupunguza ugonjwa huo kwa asilimia 40 miongoni mwa watoto.

Amesema ugonjwa wa kuhara ni ugonjwa namba tatu kusababisha vifo vingi zaidi vya watoto nchini Uganda huku karibu watoto 30 wakiwa wanafariki dunia kwa siku kote nchini.