Tutumie busara za Mandela kukabili changamoto za sasa- Guterres
Umoja wa Mataifa leo umepitisha azimio la kumuenzi Nelson Mandela kutokana na mchango wake katika kusongesha utu, amani na haki za binadamu siyo tu nchini mwake bali duniani kote kwa ujumla. Taarifa zaidi na Grace Kaneiya.
Tukio la kumuenzi Mzee Mandela lilianza kwa Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa kukabidhi sanamu ya mzee Mandela kwa Umoja wa Mataifa.
Kisha hatua muhimu ndani ya ukumbi wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa ya kupitisha azimio la kumuenzi Mzee Mandela likiangazia mchango wake wa kutetea haki za msingi za binadamu, amani na kutatua migogoro yote iliyopo duniani kwa kutumia njia za amani.
Rais wa Baraza Kuu Maria Fernanda Espinosa akahoji na kutangaza kuwa azimio limepitishwa..
Na ndipo Katibu Mkuu Antonio Guterres akahutubia hadhira hiyo iliyoleta pamoja viongozi wa nchi na wakuu wa serikali, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa akisema leo wanamkumbuka Mandela, mtu wa busara ya hali ya juu ambaye alisongesha masuala yaliyo msingi wa Umoja wa Mataifa , "Alithamini jamii iliyo huru na ya kidemokrasia ambamo kwayo watu waliishi pamoja kwa usawa na amani. Alikabilia na watesi wake mahakamani, akitambua kuwa walikuwa na nguvu ya uhai na kifo chake na katu hakurudi nyuma.”
Na kama hiyo haitoshi, Guterres akasema kuwa "Na kila pahali, alikuwa bingwa wa amani, kusamehe, unyenyeku, upendo, utu na haki za binadamu."
Na kwa mantiki hiyo Guterres amesema katika zama za sasa zenye tishio la haki za binadamu na amani “Tunahitaji kukabiliana na mashinikizo haya kwa kutumia busara, ujasiri na uthabiti aliokuwa nao Mandela.”