Kimbunga Mangkhut chaleta maafa Ufilipino, Guterres atuma rambirambi
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameeleza masikitiko yake makubwa kufuatia ripoti za vifo vya watu vilivyosababishwa na kimbunga Mangkhut nchini Ufilipino.
Vyombo vya habari vinaripoti kuwa kimbunga hicho Mangkhut ambacho kilipiga Ufilipino siku ya jumamosi hadi sasa kimesababisha vifo na maafa mengine makubwa ambapo maiti zaid iya 40 wameshafukuliwa kutoka kwenye vifusi.
Kutokana na maafa hayo, Katibu Mkuu kupitia taarifa iliyotolewa na msemaji wake hii leo mjini New York, Marekani ametuma salamu za rambirambi kwa familia za waliopoteza maisha pamoja na serikali ya Ufilipino.
Amepongeza uongozi wa kitaifa na wa majimbo nchini Ufilipino kwa hatua walizochukua kujiandaa na kuchukua hatua kusaidia jamii zenye mahitaji.
Katibu Mkuu amesema Umoja wa Mataifa nchini Ufilipino huko tayari kushirikiana na kusaidia jitihada zinazoongozwa na serikali dhidi ya zahma hiyo na uko tayari kuongeza msaada iwapo utaombwa kufanya hivyo.
Kimbunga hicho Mangkhut baada ya kupiga Ufilipino kimeripotiwa kuelekea pwani ya kusini mwa China ambako nako kimefanya uharibifu mkubwa.