Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kafando ahitimisha ziara Burundi aelekea Dar es salaam

Mjumbe mpya maalumu wa katibu Mkuu wa Umoja wa mataifa nchini Burundi Michel Kafando. Picha: UM/Ky Chung

Kafando ahitimisha ziara Burundi aelekea Dar es salaam

Amani na Usalama

Mjumbe  Maalumu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa  nchini Burundi   Michel Kafando amehitimisha ziara yake ya wiki nzima nchini humo iliyomkutanisha na  wawakilishi  wa serikali, vyama vya siasa na mashirika ya kiraia ambapo amewachagiza washiriki kwenye  awamu mpya ya mazungumzo ambayo yanatarajiwa kuitishwa mwishoni mwa mwezi huu  yakisimamiwa na Jumuiya ya Afrika ya Mashariki. Mwandishi wetu wa maziwa makuu Ramadhani KIBUGA ametutumia taarifa hii kutoka Bujumbura, Burundi.

Kulingana na taarifa  ofisi ya Umoja wa mataifa hapa Burundi,  Mjumbe huyo wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Michel  Kafando alikuwa na mazungumzo na  Waziri wa mambo ya nje  na kuangazia  ushirikiano  kati ya Burundi na Umoja wa mataifa   pamoja na ushiriki wa  serikali kwenye raundi mpya  ya mazungumzo  yanayosimamiwa na Jumuiya ya Afrika ya mashariki.

Kwenye  ziara  hiyo,  Bwana Kafando alikuwa pia  na vikao kwenye nyakati tofauti na wakuu wa   chama tawala na washiriika wake wa karibu   pamoja na  wapinzani wakiongozwa Muungano wa  Amizeri Y’ Abarundi.

Taarifa hiyo inasema walizungumza maendeleo ya kisiasa nchini Burundi , ikiwemo uitishwaji wa  raundi ya tano ya mazungumzo . Kwa Mujibu wa Kafando , pande zote mbili zimethibitisha azma ya  kushiriki  kwenye mazungumzo hayo  kukiwa na matumaini ya kufikia  maelewano ya kumaliza mgogoro  unaoikabili Burundi.

 Wanawake wa Burundi wanachangamoto. Mfano hawa walikimbilia Jamhuri ya kidemokrasia ya CongoDRC
PICHA: UNHCR/Maktaba/Eduardo Soteras Jalil
Wanawake wa Burundi wanachangamoto. Mfano hawa walikimbilia Jamhuri ya kidemokrasia ya CongoDRC

Mjumbe huyo maalumu wa Umoja wa Mataifa  alikutana pia na wawakilishi wa  mashirika ya wanawake na kuzungumzia ushiriki wa wanawake sawa na  mashirika ya kiraia kwenye raundi  hiyo mpya  ya mazungumzo.

Mwanadiplomasia huyo amejadiliana  pia na wawakilishi wa jumuiya ya kimataifa  wakiwemo katibu mkuu wa Kongamano la maziwa makuu CIRGL, mwakilishi wa Muungano wa afrika, mabalozi,   pamoja na  mashirika ya Umoja wa Mataifa. Mbali na maswala  kuhusu mazungumzo, wamezungumzia pia   hali ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii   ya Burundi.

Kwenye taarifa hiyo,  Bwana Kafando amesema alikuwa na mazungumzo  mazuri na ya  kufana  na wadau mbalimbali wa siasa za Burundi.  Amewachagiza  wanasiasa wote kushiriki vikao hivyo  na  kufikia makubaliano katika raundi  hiyo ijayo  ya mazungumzo . Pia ameomba  Jumuiya ya Kimataifa kuendelea kuisapoti  Burundi katika juhudi zake za maendeleo.

Mjumbe maalumu  wa katibu Mkuu Michel Kafando ameondoka Bujumbura jumatano hii na kuelekea Dar Es Salaam Tanzania ambako  atakuwa pia  na  mashauriano  na  msuluhishi katika mgogoro wa Burundi  Benjamin Mkapa.