Suala la ukatili dhidi ya watoto Sudan Kusini lishughulikiwe haraka: Virginia Gamba.
Ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu dhidi ya watoto nchini Sudan Kusini umesalia kuwa katika kiwango cha juu kisichokubalika huku takriban watoto 1,400 wakithibitishwa kuwa wahanga wa moja kwa moja wa ukiukwaji huo kwa mwaka 2017 na maelfu wengine wakiendelea kuteseka.
Onyo hilo limetolewa leo mjini Juba, nchini sudan Kusini , na Mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anaehusika na watoto katika migogoro ya silaha,Bi Virginia Gamba, baada ya kukamilisha ziara yake ya siku nne nchini humo.
“Nina wasiwasi kubwa kuhusu kiwango cha ukatili dhidi ya watoto hususan katika mikoa ya Upper Nile na Unity. Katika mikoa hiyo miwili ukatili dhidi ya watoto uliyoripotiwa unajumulisha asilimia 60 au zaidi ya matukio yote ya nchi nzima.”
Bi Gamba amesema kutokana na hali hiyo, amehimiza suala la dhulma dhidi ya watoto nchini Sudan Kusini livaliwe njuga ili kuhakikisha uwajibikaji na pia kuzuia hali kama hiyo kutojitokeza tena siku za usoni. Na kusema Umoja wa Mataifa uko tayari kusaidia utekelezaji wa hatua hizo na pia kutoa msaada wa kiufundi .
Amefafanua kuwa ukatili dhidi ya watoto ni moja ya aina sita za ukiukwaji ambazozinashughulikia katika Umoja wa Mataifa.
Ameongeza kuwa watoto wengi nchini humo wameteseka kiasi cha kutosha naameziomba pande zote katika mzozo wa Sudan Kusini kuhakikisha zinawalinda watoto dhidi ya athari za vita kwani asilimia 50 ya watu wote wa taifa hilo ni watoto walio chini ya umri wa miaka 18.
Pia amezihimiza pande zote husika kuendelea kuwaachilia huru watoto kutoka katika kazi ya kubeba silaha na kuwashirikisha vitani akisema anaunga mkono na kufurahishwa na hatua ya mwaka huu ya kuachiliwa kwa watoto mwaka 2018 .
Katika ziara hizo alitembelea pia Yambio, katika eneo la Western Equatoria ambako alikutana na Gavana na kufanya mazungumzo mjini Juba na makamu wa rais wa kwanza ,Taban Deng Gai na vilevile vigogo wengine.