Vikwazo vya kiuchumi dhidi ya Iran vinaumiza, asema mtaalam wa UN
Vikwazo vinafaa kuwa vya haki na visisababishie mateso wananchi wa kawaida , amesema mtaalam maalum wa Umoja wa Mataifa Idriss Jazairy katika taarifa iliyotolewa leo na ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa, mjini Geneva, Uswisi.
Bw Jazairy ambaye ni mtaalamu maalum kuhusu vikwazo vinavyozuia watu kufurahia haki zao za msingi, amebaini kuwa kurejeshea tena Iran vikwazo baada ya Marekani kujiondoa kutokamakubaliano ya mpango wa nyuklia wa Iran, ambayo yaliidhinishwa na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa na kuungwa mkono na Marekani yenyewe, ni ishara tosha kuwa hatua ya Marekani si halali.
Ukosefu wa uhalali wa kisheria wa hatua hiyo, ulithibitishwa na hatua ya wajumbe wa kudumu wa Baraza la Usalama kupinga hatua ya Marekani, sambamba na wadau wote wa kimataifa.
Ameongeza kuwa vikwazo vya kimataifa, ni lazima viwe na sababu ya kisheria na havipaswi kuumiza haki za binadamu za raia wa kawaida, na hakuna hata kigezo kimoja kati ya hivyo kilichotumiwa katika vikwazo hivyo.
Bw Jaizairy anasema kuwa vikwazo hivyo vinaumiza uchumi na sarafu ya Iran na kuwasukuma mamilioni kadhaa ya watu kwenye umaskini na vilevile kufanya bidhaa zinazoagizwa kutoka nje kuwa vya gharama, akihoji endapo Marekani itatoa chakula na dawa kwa mamilioni ya wairan ambao sasa hawawezi kukidhi mahitaji yao.
“Nasihi Marekani ionyeshe nia yake ya kuruhusu bidhaa za kilimo, chakula,, dawa na vifaa vya matibabu viingie nchini Iran kwa kuchukua hatua madhubuti za kuhakikisha benki na taasisi za fedha na kampuni zinaweza kuwa na uhakika wa kuingiza bidhaa na malipo yao yataruhusiwa,” amesema Bwana Jaizairy.
Vikwazo hivi pamoja na matukio ya hivi karibuni vimesababisha mtaalam kuonya dhidi ya vita jumuishi vya kiuchumi duniani.