Misaada ya kibinadamu yasababisha mapigano Kuda Sudan Kusini
Kuelekea siku ya usaidizi wa kibinadamu duniani tarehe 19 mwezi huu wa Agosti, ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini umeanza kuchunguza mauaji ya watu 14 waliouawa wakati wa mapigano baina ya jamii za wafugaji nje ya Juba, mji mkuu wa nchi hiyo.
Hapa ni Kuda, kijiji kilichopo kilometa 72 kusini mwa mji mkuu wa Sudan Kusini, Juba.
Wanaonekana maafisa wa UNMISS wakionyeshwa moja ya makaburi mapya kabisa, walikozikwa watu hao 14 waliotokana na mapigano.
Wanawake na watoto wanakimbia makazi yao na kaya takribani 600 zimesaka hifadhi kwenye chumba cha darasa la shule moja ya msingi.
Grace Yangi ni miongoni mwao..
“Hakuna chakula, tunasikia njaa. Tunakula majani baada ya kuyachemsha. Hamna chumvi hamna mafuta wala siagi ya karanga.Macho ya watoto wetu yanavimba. Hali yetu ni mbaya sana. Tunategemea haya majani. Huwatunawagawia watoto kwenye sahani na wanakula. Hebu nitazame, sina hata maziwa ya kumpatia mtoto.”
Kumekuwepo ripoti za ghasia kufuatia madai ya kwamba jamii moja ilishambulia nyingine kwa lengo la kuiba misaada ya kibinadamu iliyotolewa na shirika la Umoja wa mataifa la mpango wa chakula la WFP.
Masmina Munga ni afisa wa masuala ya kiraia wa UNMISS na anafafanua kwa nini raia hao wanaomba msaada wa chakula …
“Wanaomba chakula kwa sababu hivi sasa wako hapa, lakini wameacha chakula kule walikotoka. Wanataka kufuata chakula chao lakini hali bado ni tete huko na wanaweza kuviziwa na magenge ya watu wenye silaha waliowashambulia awali. Hofu yao ni kwamba iwapo wataenda huko watauawa hivyo ni kheri ikiwa watapewa msaada hapa.
Wakati Sudan Kusini bado inaonekana kuwa ni moja ya maeneo hatari kwa wahudumu wa misaada kufanya kazi zao, walinda amani wa UNMISS wanaendelea na doria iwe ni katika ziara za kutathmini hali ya usalama au ulinzi kwa lengo la kuweka mazingira bora na salama.