Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wafanyakazi wanaosafisha mtambo wa Fukushima Daiichi wanadhulumiwa

Wataalam wa IAEA wakikagua kinyapuzi namba 3 katika kinu cha  nishati ya Nyuklia  Fukushima Daiichi Japan
Photo: IAEA/Giovanni Verlini
Wataalam wa IAEA wakikagua kinyapuzi namba 3 katika kinu cha nishati ya Nyuklia Fukushima Daiichi Japan

Wafanyakazi wanaosafisha mtambo wa Fukushima Daiichi wanadhulumiwa

Afya

Japan ichukue hatua haraka kulinda makumi ya maelfu ya wafanyakazi wanaoripotiwa kudhulumiwawakati wanafanya kazi ya kusafisha mtambo wa nyuklia ulioharibika wa Fukushima Daichi.

Hayo yamesemwa na wataalamu watatu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa katika taarifa yao iliyotolewa mjini Geneva, Uswisi hii leo, wakisema kuwa wafanyakazi  hao wanakabiliana na minururisho ya nyuklia  yenye sumu.

Wataalam hao wamesema  wafanyakazi hao walioajiriwa kusafisha  mtambo huo wa Fukushima Daiichi ni wahamiaji, wasaka-hifadhi pamoja na watu wasio na makazi.

 

Kinu cha nishati ya Nyuklia cha Fukushima kikiwaka moto kufuatia tetemeko kubwa la ardhi pamoja na Tsunami vya mwaka 2011 nchini Japan.
UN Photo.
Kinu cha nishati ya Nyuklia cha Fukushima kikiwaka moto kufuatia tetemeko kubwa la ardhi pamoja na Tsunami vya mwaka 2011 nchini Japan.

Hofu yao wataalamu hao ni kwamba wafanyakazi hao wanaweza kuwa wamehadaiwa juu ya hatari zitokanazo na minururisho wakati wa kusafisha mtambo huo, wameshinikizwa kukubali kufanya kazi katika   mazingira hatari kutokana na hali ngumu ya kiuchumi inayowakabili au hawana mafunzo ya kujikinga.

Na zaidi  ya yote wanasema “ripoti za kina zinaonyesha kuwa kandarasi ya kuondoa sumu kwenye eneo la mtambo zilipatiwa wakandarasi wakubwa na kwamba kampuni mamia ya kampuni ndogo yasiyo na uzoefu yalipatiwa kandarasi ndogo za kusaka watu wa kufanya kazi hiyo kupitia madalali, hali ambayo inaweza kuwa iliweka mazingira bora ya kudhulumu wafanyakazi na kukiuka haki zao.”

Kwa kuzingatia hilo, wataalamu hao wana hofu juu ya madhara ya minururisho hiyo kwa afya za mwili na akili za wafanyakazi hao.

 

Uharibifu katika kinu cha nishati ya Nyuklia cha Fukushima Daiichi uliosababishwa na  tetemeko la ardhi pamoja na Tsunami vya  2011.
Photo: IAEA/Gill Tudor
Uharibifu katika kinu cha nishati ya Nyuklia cha Fukushima Daiichi uliosababishwa na tetemeko la ardhi pamoja na Tsunami vya 2011.

 

Uchafuzi wa eneo hilo na kuenea kwa minururisho ya nyuklia vinasalia kuwa ni hatari kubwa kwa wafanyakazi wanaojaribu kulifanya liwe salama tena, miaka saba baada ya mtambo huo kusambaratikakutokana na tetemeko la ardhi lililofuatiwa na tsunami.

Kwa kipindi cha miaka saba sasa, mamia ya maelfu ya wafanyakazi wameajiriwa ili kusafisha eneo hilo chini ya mpango maalum wa kuondoa sumu hiyo.

Katika wavuti wake wizara ya  Afya, Kazi na Maslahi nchini Japan inaonyesha kuwa wafanyakazi  46,386 waliajiriwa mwaka 2016,  huku kituo cha kusajili wafanyakazi wahusikao na masuala ya minururisho nchini humo kilionyesha kuwa kiliajiri watumishi 76,951 katika kipindi cha miaka mitano hadi mwaka 2016.