Urusi muachilieni haraka mtengenezaji filamu wa Ukraine: UN
Wataalam wa Umoja wa Mataifa wamezitaka mamlaka nchini Urusi zimuachilie huru mara moja na bila masharti Oleg Sentsov, huku wakielezea wasiwasi wao kuhusu hali yake ya kiafya kwa sasa.
Olego Sentsov, mtengenezaji wa filamu raia wa Ukraine na mkosoaji mkuu wa hatua ya Urusi ya kukalia kwa nguvu eneo la Crimea, alikamatwa mwezi mei mwaka 2014 na kuhukumiwa kifungo cha miaka 20 kwa kosa la ugaidi, kama raia wa nchi hiyo.
Kupitia taarifa yao waliyotoa leo mjini Geneva Uswisi, watalaam hao wamesema “maisha ya Sentsov yako hatarini. Mgomo wake aliouanza unafuatia hukumu ambayo ina mapungufu ya kiwango cha sheria za kimataifa na tunazitaka mamlaka za Urusi zimuachie haraka bila masharti yoyote.”
Miezi mitatu iliyopita alianza mgomo wa kula chakula akipinga kile anachoamini kuwakufungwa jela kwa raia 64 wa Ukraine nchini Urusi kwa sababu za kisiasa.
Watalaam wa Umoja wa Mataifa wametoa wito kwa serikali ya Urusi kuhakikisha kuwa, Bwana Sentsov anapewa matibabu anayohitaji haraka na ambayo yanatokana na idhini yake.
Tayari wataalamu hao wanawasiliana na serikali hiyo kuhusu kesi yake hii.