Tunaunga mkono harakati za kuwa na rasi ya Korea isiyo na nyuklia- Guterres

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres aliyepo ziarani nchini Japan amesisitiza azma ya chombo hicho ya kutokomeza matumizi ya silaha za nyuklia duniani.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Tokyo, Japan katika mkutano uliohudhuriwa pia na Waziri Mkuu wa nchi hiyo Shinzo Abe, Bwana Guterres amesema ni kwa mantiki hiyo anaunga mkono mazungumzo yanayoendelea ili kutokomeza silaha hizo akitolea mfano mashauriano kati ya Marekani na Jamhuri ya kidemokrasia ya watu wa Korea, DPRK ijulikanayo pia kama Korea Kaskazini.
Sauti ya Antonio Guterres
“Ninaunga kuunga mkono kikamilifu mazungumzo yanayoendelea kati ya Marekani na na Jamhuri ya watu wa Kidemokrasia ya Korea DPRK yenye lengo ambalo sisi sote tunalikubali la kuona utokomezaji wa nyuklia unaoweza kuthibitishwa na kuhakikisha kwamba Korea ya Kaskazini inaweza kuwa mwanachama wa kawaida jumuiya ya kimataifa katika ukanda huu” .
Bwana Guterres amesema wanaunga mkono pia harakati za Japan za mazungumzo na Korea Kaskazini akisema na ndio maana mwezi Mei mwaka huu huko Geneva, Uswisi walizindua mkakati wa kuondokana na silaha za nyuklia ulimwenguni, mkakati ambao amesema unalenga kuokoa maisha ya binadamu.
Ametumia fursa hiyo pia kuishukuru Japan kwa uongozi wake katika suala la kutokomeza silaha duniani, kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi pamoja na uendelezaji wa haki za binadamu na masuala shughuli nyingine zinazopigiwa chepuo na Umoja wa Mataifa.
Kesho Alhamisi Katibu Mkuu atashiriki katika kumbukizi ya miaka 73 tangu shambulio la bomu la atomiki kwenye mji wa Nagasaki nchini Japan.