Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Heko Hibakusha kwa kuchagiza dunia bila nyuklia- Guterres

Katibu Mkuu UN António Guterres akitoa hotuba kwenye jukwaa wakati wa hafla ya Kumbukumbu ya Amani ya Nagasaki nchini Japan.
UN Dan Powell Katibu Mkuu wa UN António Guterres akisoma hotuba yake kwenye kumbukizi ya shambulio la bomu huko Nagasaki nchini Japani

Heko Hibakusha kwa kuchagiza dunia bila nyuklia- Guterres

Amani na Usalama

Umoja wa Mataifa umesema hibakusha, ambao ni manusura wa mashambulio ya mabomu ya nyuklia huko Nagasaki na Hiroshima nchini Japan wamesalia kuwa viongozi wa amani na udhibiti wa kuenea silaha hizo nchini humo na duniani kwa ujumla.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema hayo leo huko Nagasaki nchini Japan katika kumbukizi ya miaka 73 tangu Marekani iangushe bomu la atomiki lililoua maelfu ya watu na wengine kusalia na majeraha ya kudumu.

“Wanatambuliwa siyo kwa miji yao ambayo ilisambaratishwa, bali kwa dunia yenye amani ambayo wanaisaka,” amesema Bwana Guterres akiongeza kuwa Hibakusha wamepaza sauti zao kwa niaba ya binadamu wote na hivyo ni lazima kuwasikiliza.

Bwana Guterres amesema licha  ya sauti hizo kupazwa na mikataba ya kimataifa kupitishwa ili kudhibiti kuenea kwa silaha hizo hatari, bado mataifa yanaendelea kutengeneza na kupanua umiliki wao wa silaha hizo.

Mwanamume mzee aliyevaa koti la kahawia akizungumza na hadhira iliyoketi katika chumba cha mikutano.
UN/Jihye Shin Tarehe 18 disemba 2015, Yasuaki Yamashita, mmoja wa manusura wa shambulio la Nagasaki wajulikanao kama Hibakusha kwa kijapan na ambaye sasa anaishi Mexico, alikuwa na mazungumzo na wafanyakazi wanatoa huduma za ziara ndani ya UN, jijini New York, Marekani

“Serikali zinazomiliki silaha za nyuklia zinatumia kiasi kikubwa cha fedha kuziboresha. Zaidi ya dola trilioni 1.7 zilitumika mwaka 2017 kwenye silaha, ikiwa ni kiwango cha juu zaidi tangu kumalizika kwa vita baridi. Kiasi hicho in mara 80 zaidi ya fedha zinazohitajika kwa misaada ya binadamu duniani,” amesema Katibu Mkuu.

Amesema suala la kuondokana na silaha ni kipaumbele cha juu zaidi cha Umoja wa Mataifa na hivyo ametumia hadhira ya Nagasaki kutoa wito kwa nchi zote kuazimia kuondokana na silaha za nyuklia.

Katibu Mkuu UN Ban Ki-moon akiweka shada la maua katika Mnara wa Hypocenter katika Hifadhi ya Amani ya Nagasaki.
UN /Eskinder Debebe Eneo la kitovu cha bomu la nyuklia huko Nagasaki sasa pamejengwa mnara wa amani.

“Hebu Nagasaki na Hiroshima zitukumbushe kupatia amani kipaumbele kila siku, kufanya kazi za kuzuia mizozo, kuweka maridhiano na mazungumzo na kushughulikia mizizi ya mizozo na ghasia,” amesema Bwana Guterres.

Ametaka kila mtu kuazimia kuwa Nagasaki ni eneo la mwisho duniani kukumbwa na shambulio la nyuklia akisema yeye atashirikiana nao kufanikisha azma hiyo.

Shambulio la Nagasaki lilifanyika siku mbili baada ya lile la Hiroshima.

Katibu Mkuu UN António Guterres akikunja korongo za asili na viongozi vijana wa Japani katika Ukumbusho wa Amani wa Nagasaki.
UN/ Dan Powell Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres akishirikiana na watoto wa kijapani kukunja korongo kwa kutumia karatasi, kwenye mnara wa amani Nagasaki. Huu ni utamaduni wa kipekee kwa Japani.