Mazungumzo ya amani ya Yemen kuanza Geneva mwezi ujao- Griffiths
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limekutana hii leo mjini New York, Marekani kujadili kuhusu Yemen ambapo wajumbe wamejulishwa kuwa awamu ya kwanza ya mazungumzo baina ya pande kinzani itafanyika tarehe 6 mwezi ujao mjini Geneva, Uswisi.
Mjumbe maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwa Yemen, Martin Griffiths ametangaza tarehe hiyo akiwasilisha mapendekezo yake mbalimbali kusuhu jinsi ya kumaliza mzozo wa Yemen uliodumu kwa zaidi ya miaka mitatu sasa.
Bwana Griffiths amesema amefikia hatua hiyo baada ya mashauriano na pande zote husika nchini Yemen, ikiwemo pande kinzani, mashirika ya kiraia na kwamba bado anaendelea na mashauriano na pande nyinginezo.
Kwa mantiki hiyo ameomba wajumbe wa Baraza la Usalama kuunga mkono jitihada zake za kufanikisha mazungumzo hayo yatakayofanyika mjini Geneva.
Pili wajumbe wasaidia kufanikisha kusitisha mapigano yanayoendelea kwenye bandari ya Hudaidah na kuepusha bahari ya Sham dhidi ya mgogo huo wa Yemen.
Bwana Griffiths pia ametaka kuungwa mkono kwa hatua ambazo zinarejesha matumaini kwa wananchi wa Yemen.
Akizungumzia hali halisi nchini Yemen hivi sasa hususan matumizi ya bandari ya Hudaidah ambayo Umoja wa Mataifa iliafikiana na Ansar Allah kiongozi wa wapiganaji wa kihouthi , Bwana Griffiths amesema bado kuna mkwamo kwenye kufanikisha makubaliano kati yao.
“Tutaendelea na juhudi zetu za kupata ufumbuzi wa amani kwa Hudaidah. Mafanikio haya yanatokana na ushirikiano mkubwa kutoka pande zote na msaada wa Baraza hili. Ninaendelea na ushirikiano wa karibu na serikali ya Yemeni pamoja na viongozi wa washirika kwenye mzozo huo. Pia Nimekuwa na mfululizo wa mikutano yenye tija na uongozi wa ngazi ya juu wa Ansar Allah naamini huu ni ufunguo wa mafanikio yoyote katika jitihada hii,” amesema mjumbe huyo maalum wa Umoja wa Mataifa kwa Yemen.
Bwana Griffiths amegusia pia mazungumzo yake na Rais Abdrabbuh Mansur Hadi wa Yemen kuhusu suala la kuachia huru wafungwa wa kivita, hoja ambayo inapigiwa chepuo na pande zote kinzani nchini humo.
Amesema Rais Hadi ameunga mkono hoja hiyo akimsihi aifanikishe na kwamba ikamilishwe kabla ya mkutano wa Geneva.
Mkutano kuhusu mchatako wa amani wa Yemen ulianzishwa miaka 2 iliyopita chini ya uongozi wa mfalme Sheikh Jaber al-Ahmad al-Sabah wa Kuwait ambaye alijenga msingi wa mazungumzo yanayoendela hivi sasa .