Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Bei ya vyakula mwezi Julai imeshuka: FAO

Biashara ya nafaka nchini Sierra Leone. Picha: FAO/Sebastian Liste_NOOR

Bei ya vyakula mwezi Julai imeshuka: FAO

Ukuaji wa Kiuchumi

Bei ya vyakula kimataifa imeshuka mwezi wa Julai kwa mujibu wa shirika la chakula na kilimo FAO linalofuatilia mwenezo wa bei hizo kila mwezi.

Katika data zake za Julai FAO inasema vuyakula vyote muhimu kama nafaka, bidhaa za maziwa, sukari, nyama na mafuta ya kupikia yatokanayo na mbogamboga vimeorodhesha kushuka kwa bei sokoni vikiongozwa na bidhaa za maziwa na sukari.

Orodha hiyo inaonyesha kwamba kwa wastani bei imepugua kwa pointi 168.8 sawa na asilimia 3.7 ikilinganishwa na mwezi wa Juni, na Julai ndio mwezi ambao umekuwa na punguzo kubwa la bei kwa mwezi tangu mwishoni mwa mwaka jana, ukizinmgatia kwamba bei imekuwa ikiongezeka mfululizo mwaka huu 2018 kuanzia Januari hadi Juni.

Bidhaa za maziwa zinaoongoza kwa kupungua bei kwa asilimia 6.6, ambapo siagi na jibini ndivyo vilivyoporomoka zaidi ya bidhaa zingine kama maziwa halisi  ya maji na maziwa ya unga.

Kwa upande wa sukari imeshuka bei kwa asilimia 6, ikichangiwa na kuboreshwa kwa uzalishaji nchini India na Thailand nchi zote muhimu kwa uzalishaji wa sukari. Lakini uzalishaji hafifu Brazili nchi ambayo ni mzalishaji na msafirishaji mkubwa wa sukari kimataifa kumedhibiti upunguaji wa bei ya sukari kimataifa.

Kwa upande wa nafaka , bei ya ngano na mahindi zimepungua kwa asilimia 3.6, huku mafuta ya kupikia bei ikiporomoka kwa alimilia 2.9 na nyama imeshuka kwa asilimia 1.9 kutokana na mgomo wa madereva wa malori ya kusafirisha nyama kutoka Brazil.

TAGS:FAO, bei ya vyakula, nyama, maziwa, sukari nafaka