Watu wenye ulemavu wahusishwe katika juhudi za kuwaendeleza:Amina
Ahadi za serikali mbalimbali kuheshimu haki za watu wenye ulemavu zimeimarishwakufuatia kupitishwa kwa ajenda ya maendeleo endelevu ya 2030 ya Umoja wa Mataifa na pia kutokana kuwepo kwa mkataba wa Umoja wa mataifa kuhusu haki za watu wenye ulemavu kuidhinishwa na kuingia katika vipengee vya haki za binadamu mkataba ambao kwa sasa umeridhiwa kote duniani.
Hayo yamesemwa na Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Bi Amina J.Mohammed, hii leo mjini London Uingereza wakati wa mkutano kuhusu watu wenye ulemavu.
Bi. Mohammed amesema kwa masikitiko ahadi hii ya kisiasa mara kadhaa inapuuzwa hususani kwa maisha ya watu takriban milioni 1.5 wenye ulemavu duniani.
Ameongeza kuwa wengi wa watu hao, bila kujali wapi waliko pamoja na uwezo wao bado wanabaguliwa na, hasa katika mataifa yanayoinukia na kuwakosesha haki zao zamsingi kama vile elimu, huduma za afya na pia kunyimwa haki ya kushiriki katika masuala mbalimbali ya kijamii.
Bi. Amina amesema mkutano huo ni fursa nzuri ya kutafuta njia za kubadili hali hiyo wakati huu wa utekelezaji wa ajenda ya 2030 ya maendeleo endelevu kwakuwajumuisha watu wenye ulemavu.
Akiunga mkono hoja hiyo katika mkutano , mratibu wa ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya binadamu OCHA, Mark Lowcock, amesema wakati huu kuna changamoto kubwa za hatua za kuhakikisha mahitaji ya kibinadamu yanaweza kumfikia kila mtu kwani hivi sasa watu zaidi ya milioni 130 duniani wanahitaji msaada wa kibinadamu na asilimia 15 ya watu hao ni wenye ulemavu, hivyo akatoa rai ,“tutaomba msaada kutoka katika mashirika ya watu wenye ulemavu ili kuhakikisha kuwa masuala ya watu wenye ulemavu yanajumuishwa katika kila ngazi ya mipango ya kibinadamu.”
Pia amesema migogoro mbalimbali pamoja na mabadiliko ya tabia nchi , vimesababisha watu zaidi ya milioni 30 kuachwa bila makazi na kati ya hao theluthi moja ni watu wenye ulemavu.
Kwa mantiki hiyo amesema, watu wenye ulemavu wanahitaji kupewa sauti ili waweze kutambua mahitaji yao wenyewe na kuahidi kuwa ofisi yake itashauriana na makundi ya watu wenye ulemavu ili kuhakikisha kuwa masuala yanayaowahusu yanajumuishwa katika mipango ya utoaji wa misaada ya kibinadamu.