Baada ya kutenganishwa na vita hatimaye mama na mwana wakutanishwa tena Ujerumani
Baada ya miaka mitatu ya upweke na kusali kutwa kucha, kijana mkimbizi wa Syria aliepata hifadhi nchini Ujerumani, dua zake zajibiwa, alipoungana tena na familia yake iliyokuwa Ugiriki
Numeir mwenye umri wa miaka 18 mkimbizi kutoka Syria alibahatika kupata hifadhi ya kudumu nchini Ujerumani kwa msaada ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR.
Akiwa nyumbani kwake akiandaa mahali watakapofikia wazazi wake, Numeir anakumbuka madhila aliyopitia akiwa ugenini mbali na familia yake.
Sauti ya Numeir
Tangu nilipowaacha wazazi wangu kila kitu kilikuwa kigumu sana kwangu, kama unavyoweza kutegemea , sababu niko mbali na familia yangu.Na kikubwa zaidi ni upweke na wa kutokuwa nao.
Akisubiri kwa hamu Numeir amejawa na shauku ya kukutana tena na wazazi wake watakaowasili muda sia mrefu.
Sauti ya Numeir
Moyo wangu unadunda kwa kasi, muda si mrefu nitaonana tena na familia yangu. Hatimaye nitamuona tena mama yangu. Mama yangu ni kama mbingu kwangu . Nimemkosa kwa muda sasa., muda si mrefu nitamuona tena mama yangu.
Hatimaye umewadia wasaa uliokuwa ukisubiriwa na pande zote, Numeir anakutana ana kwa ana na familia yake, ni fuhara iliyoje? baba yake mzazi anashindwa kujizuia kwa furaha, na kueleza….
Sauti ya Baba mzazi
Mwangu aliondoka akiwa mdogo sana,aliondoka kutokana na vita na hali ngumu ya vikwazo vya kiuchumi. Nashangazwa kumuona amekua mkubwa halafu ni mrefu kuliko mimi.
Na je Mama mzaa Chema ana lipi la kusema?
Sauti ya Mama mzazi
Sasa tunaweza kusahau yaliopita, tunaanza upya, na tutaishi pamoja tena kama familia. Maisha yetu yatabadilika, hakuna tena vita wala vikwazo vya kiuchumi. Tunatarajia kuanza upya maisha yetu.Nataka kuwalea watoto wangu na kuwasomesha katika mazingira ambayo watapata elimu bora.
Akiwa ameketi bembeni ya mama yake Numeir anafunguka
Sauti ya Numeir
Nina furaha sana mama yangu akiwa ameketi pembeni yangu. Leo ni siku ya kipekee. Asilani Siwezi kuisahau.