Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mipango ya kuwaokoa wahamiaji kutoka bahari ya Mediteraani haitoshi: UNHCR

Wakimbizi na wasaka hifadhi  mamia kwa maelf wakiwa ndani ya mashua ya kuvulia samaki mda mchache kabla ya kuokolewa na wanamaji wa Italia kipindi cha nyuma.
Picha: The Italian Coastguard/Massimo Sestini
Wakimbizi na wasaka hifadhi mamia kwa maelf wakiwa ndani ya mashua ya kuvulia samaki mda mchache kabla ya kuokolewa na wanamaji wa Italia kipindi cha nyuma.

Mipango ya kuwaokoa wahamiaji kutoka bahari ya Mediteraani haitoshi: UNHCR

Wahamiaji na Wakimbizi

Shirika la kuwahudumia wakimbizi la UNHCR , linasema linakaribisha hatua za mataifa kadhaa ya Ulaya za kumaliza mgogoro wa wahamiaji 450 waliokuwa wamekwama katika baharí ya Mediterrania kutokana na kutokubaliwa na taifa lolote kuingia nchini mwao.

Tangu Jumamosi, serikali za Ufaransa,Ujerumani, Italia, Malta, Hispania na Ureno ziliafikiana  kutia nanga kwa meli hiyo nchi kavu na kwa pamoja kuwasaidia wahamiaji  hao 450, na pia kushughulikia maombi ya hifadhi endapo yatatokea.

Hii leo  mjini Geneva Uswisi, Kamishna mkuu  wa wakimbizi Fillipo Grandi amesema, “tunatumai kwamba mpango huu sasa utatekelezwa kwa uhakika na haraka pamoja na kuwaondolea jinamizi watu hawa , na huu ni mfano mzuri wa jinsi gani kushirikiana kwa pamoja , nchi zinaweza kufanya uokozi na kulinda mipaka yake huku zikitimiza wajibu wa kimataifa kuhusu wahamiaji.”

Hata hivyo, Kamishna Grandi amesema ufumbuzi huu unapaswa kwenda mbali zaidi ya kushughulikia meli na kisa kimoja kimoja.

Wasaka hifadhi  na wahamiaji wakiwa ndani ya boti ndani ya maji ya kimataifa nje ya  mwambao wa Libya mwaka 2016
UNHCR/Giuseppe Carotenuto
Wasaka hifadhi na wahamiaji wakiwa ndani ya boti ndani ya maji ya kimataifa nje ya mwambao wa Libya mwaka 2016

 

Ameongeza kuwa mipango  ya sasa ya kushughulikia suala la wahamiaji barani Ulaya haitoshi  na inapaswa kuwa ni ya suluhu ya muda mrefu yenye tija, usimamizi na mipango endelevu, la sivyo kuwasili kwa wahamiaji kutaendelea kuwa na suluhu ya muda mfupi na isioendelevu.

Wakati huohuo amesema wakati mataifa yana wajibu wa kuokoa maisha na kuwalinda wakimbizi, watu wanaookolewa hawana haki ya moja kwa moja ya kuchagua wapi wanakotaka kwenda. Wanatakiwa kutia nanga mahali ambapo pana usalama , ikiwa ni pamoja na wale watakaohitaji ulinzi wa kimataifa , lakini sio lazima ikiwa ni mahali wanapopondelea.