“Madiba” akumbukwa kwa uvumilivu wake- Guterres
Leo ni kumbukizi ya miaka 100 tangu kuzaliwa kwa Rais wa kwanza mwafrika wa Afrika Kusini, hayati Nelson Mandela.
Umoja wa Mataifa katika kuadhimisha siku hiyo imesema inamkumbuka kwa harakati zake za kupigania haki na usawa na zaidi ya yote kuendelea kuleta msukumo duniani kupitia mifano yake wa ujasiri na huruma.
Katika ujumbe wake wa siku hii inayoadhimishwa tarehe 18 Julai kila mwaka, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema.
(SAUTI YA ANTONIO GUTERRES)
“Nelson Mandela alikuwa mateka kwa miaka mingi, lakini hakuwa mfungwa wa yaliyomfika. Badala yake alitumia nguvu zake katika kusameheana pamoja na kuona hali ya baadaye ya Afrika Kusini yenye amani, makabila tofauti na ya kidemokrasia.”
Bwana Guterres ameongeza kuwa ingawa amefariki dunia bado mchango wake unatambulika akisema.
(SAUTI YA ANTONIO GUTERRES)
“ Hakuna mtu ambaye katika historia yake amewahi kufanya mengi kuchochea ndoto za watu wengi na kuwafanya waweke vitendo ndoto zao.Na mapambano ya usawa,heshima na haki yanaendelea.”
Maadhimisho ya siku ya leo yaliasisiwa na azimio la Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa la mwezi Novemba 2009 ambalo lilitangaza siku hii kama ya kimataifa na hiyo ni kutokana na kazi zake za kuleta amani na uhuru.
Mandela akitambulika pia kama Madiba, anakumbukwa kwa kujitolea kwake kutatua migogoro,kuboresha uhusiano baina ya watu wenye asili na rangi tofauti ,kusamehe wengine, kuboresha haki za binadamu, kuendeleza usawa wa kijinsia, kupambana dhidi ya umasikini na mengine mengi.
Watu wengi husherehekea siku hii kwa kufanya kazi za kujitolea kwa dakika sitini na saba, kama vile kufyeka majani sehemu za umma na mambo mengine ya kujitolea.