Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ndege zisizo na rubani kudhibiti uvuvi haramu Afrika

Ndege zisizo na rubani hupachikwa programu ambazo zinafuatilia masuala  yanayoathiri ustawi wa binadamu
WeRobotics
Ndege zisizo na rubani hupachikwa programu ambazo zinafuatilia masuala yanayoathiri ustawi wa binadamu

Ndege zisizo na rubani kudhibiti uvuvi haramu Afrika

Ukuaji wa Kiuchumi

"Lengo la teknolojia hiyo si kuondokana na uwepo wa binadamu bali upekee wake ni kwamba inaweza kufanya ufuatiliaji kwenye maeneo ambayo binadamu hawezi kufika na kuamua bila kuingiliwa na mtu  yeyote."

Kampuni moja nchini Morocco imeibuka na FishGuard ambayo ni teknolojia ya kutumia ndege zisizo na rubani au drones kudhibiti uvuvi haramu na  uporaji wa maliasili barani Afrika.

Badr Idrissi ambaye ni afisa mtendaji wa kampuni hiyo ATLAN Space amesema yeyé na mwasisi mwenza wa kampuni hiyo Younes Moumen walichukua hatua hiyo baada ya kubaini kuwepo kwa uporaji mkubwa wa masiliasili hizo kuanzia baharini hadi misituni.

“Mathalani tuligundua kuwa Mauritania, Senegal, Gambia, Guinea Bissau, Guinea na Sierra Leone wanapoteza jumla ya takribani dola bilioni 2.3 kila mwaka kutokana na  uvuvi haramu,” amesema Bwana Idrissi ambaye aliacha ajira yake kwenye kampuni ya Microsoft ili kuanzisha kampuni hiyo.

Bwana Idrissi amesema walibuni program ambayo inapakizwa kwenye ndege hizo zisizo na rubani, program ambayo inaweza kufuatialia boti ya uvuvi na kubaini iwapo uvuvi unaofanyika ni halali au kinyume cha sheria.

Tuligundua kuwa Mauritania, Senegal, Gambia, Guinea Bissau, Guinea na Sierra Leone wanapoteza jumla ya takribani dola bilioni 2.3 kila mwaka kutokana na  uvuvi haramu

“Katika hiyo programu tunakuwa tumeipatia taarifa kuhusu ulinzi wa maeneo ya majini, maeneo yaliyoshamiri zaidi kwa uvuvi haramu pamoja na hali ya hewa. Pia tunaipatia taarifa za kuwezesha kutofautisha mazingira moja na mengine,” amesema Afisa mtendaji mkuu huyo wa ATLAN Space.

Amesema baada ya uchambuzi, ndege hiyo isiyo na rubani ambayo inaweza kukagua eneo la ukubwa wa kilometa 1,000 za mraba huamua iwapo iripoti tukio hilo au la.

“Iwapo itakuwa na uhakika wa asilimia 95 kuwa tukio la uvuvi linalofanyika ni haramu, basi itatuma taarifa kwa mamlaka  za eneo husika kuhusu eneo ambako chombo hicho cha uvuvi kinapatikana,” amefafanua.

“Ndege zetu hizi zinaenda eneo kubwa zaidi kwa kuwa zilizopo uwezo wake ni asilimia 70 tu ya eneo hilo, na pia zinapaa hewani kiasi kwamba haziwezi kufikiwa na chombo chochote kisicho cha kijeshi,” amesema Bwana Idrissi.

Boti nyingi za uvuvi haramu huendesha shughuli zao kwenye maeneo ambako si rahisi kufuatiliwa lakini ndege zisizo na rubani huweza kufika.
IFAD/Franco Mattioli
Boti nyingi za uvuvi haramu huendesha shughuli zao kwenye maeneo ambako si rahisi kufuatiliwa lakini ndege zisizo na rubani huweza kufika.

Amesisitiza kuwa lengo la teknolojia hiyo si kuondokana na uwepo wa binadamu bali upekee wake ni kwamba inaweza kufanya ufuatiliaji kwenye maeneo ambayo binadamu hawezi kufika na kuamua bila kuingiliwa na mtu  yeyote.

“Teknolojia yetu zaidi ya yote si ya kuchukua nafasi ya binadamu, la hasha bali inalenga kufanya kazi ya binadamu iwe bora zaidi kwani shughuli haramu zinaharibu ajira,” amesema Bwana Idrissi.

Teknolojia hiyo iendayo kwa jina la FishGuard itaanza kutumika nchini Seychelles na baadaye kuenezwa maeneo mengine huku wakiwa na mpango wa kubuni njia kama hiyo kudhibiti uporaji wa madini na mali za misitu.

Afisa habari wa shirika la mazingira  la Umoja wa Mataifa, UN Environment kwa kanda ya Afrika Mohamed Atani akizungumzia teknolojia hiyo amesema ni vyema kusaidia wajasiriamali vijana wa Afrika kwa kuwa wanachangia katika maendeleo endelevu.

Ametoa wito wa kusaka miradi mingi zaidi ya ubunifu kama FishGuard ili kupata suluhisho kwa matatizo yanayokumba bara la Afrika.