Je tumefikia wapi katika kufanikisha maendeleo endelevu- ECOSOC
Tuko hapa kutafakari tumefikia wapi hadi sasa katika mchakato wa kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu, SDGs amesema rais wa Baraza la kiuchumi na kijamii la Umoja wa Mataifa-ECOSOC, Marie Chatardova jijini New York, Marekani hii leo wakati akifungua mkutano wa ngazi ya juu wa kutathmini malengo hayo.
Ni kwa mantiki hiyo Bi Chatardova amesema kikao hicho cha ngazi ya juu kinachotoa fursa kwa nchi 47 kuwasilisha tathmini zao za utekelezji ni fursa nzuri ya kuona mafanikio ya SDGs miongoni mwa nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa.
Amesema ili kuweza kuleta mabadiliko duniani ni vyema kuhamasisha jamii, mashirika pamoja na kampuni za kibiashara bila kusahau wananchi wenyewe.
“SDGs ni sharti zitutie moyo sisi sote ili tuweze kushawishika. Ni lazima ziwe kigezo ambacho taasisi na watu watapimia ufanisi wa shughuli zao. Au zinafaa kuwa niprogramu ambazo wananchi watazitumia kuziwajibisha serikali,” amesema rais huyo wa ECOSOC.
Mkutano huo ulioanza leo katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York, utaendelea kwa siku nane ambapo wajumbe kutoka sehemu mbalimbali watabadilishana uzoefu na kutafakari kuhusu changamoto na mikingamo wanayokabiliana nayo katika kusonga mbele na SDGs