Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mchango wa wanawake ni muhimu kwa mustakabali wa Niger -Bi. Mohammed

Rais Mahamadou Issoufu wa Niger (katikati) akikaribisha ujumbe wa UN na AU akiwemo Naibu Katibu wa UN Amina  Mohammed (kushoto) kwake na waziri wa mashauri ya nje wa Sweden Margot Wallsrom,(kulia)
UN News/Daniel Dickinson
Rais Mahamadou Issoufu wa Niger (katikati) akikaribisha ujumbe wa UN na AU akiwemo Naibu Katibu wa UN Amina Mohammed (kushoto) kwake na waziri wa mashauri ya nje wa Sweden Margot Wallsrom,(kulia)

Mchango wa wanawake ni muhimu kwa mustakabali wa Niger -Bi. Mohammed

Amani na Usalama

Mchango wa wanawake katika nafasi za uongozi ni muhimu kwa mustakabali wa amani nchini Niger

Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Amina J. Mohammed amesema hayo leo huko mjini Niamey nchini Niger katika mkutano na rais wa Niger , Mahamadou Issoufu,  ikiwa ni sehemu ya ziara yake anayoambatana na viongozi wa Muungano wa Afrika, AU.

Amewaambi waandishi wa habari kuwa alimsisitizia mwenyeji wake,  umuhimu  wa wanawake kushirikiana na mamlaka katika kuzuia  migogoro.

“Pia nimetilia mkazo umuhimu wa  kuwajumulisha wanawake  katika masuala yote ya kitaifa na kikanda katika changamoto zote zinazoendelea katika Niger na eneo la Sahel kwa ujumla kama vile mazingira, kibinadamu,na kimaendeleo,” amesema Bi. Mohammed.

Wanawake wahusishwe katika ngazi zote

Naibu Katibu Mkuu  anaongoza ujumbe wa pamoja wa Umoja wa Mataifa na Muungano wa Afrika kuzuru Niger.

Shabaha kuu ya ziara hiyo ya siku mbili ni ushirikishwaji wa wanawake katika juhudi za kuzuia migogoro pamoja na udhibiti wa misimamo mikali.

Suala la usalama

Hali ya usalama nchini Niger, iliharibika kuanzia mwaka 2015 wakati kundi la Boko Haram lilipofanya sambulio la kwanza huko Diffa mashariki mwa nchi hiyo, na kusababisha takriban watu 300,000 kupoteza makazi yao wengi wao wakiwa ni watoto na wanawake.

Kuwepo kwa kundi la Boko Haram, ambalo lina nia ya kuunda taifa la kiislamu kaskazini mwa Nigeria, kumeleta madhara makubwa kwa wanawake na wasichana ambao wamepitia kile Umoja wa Mataifa unachoita, “ukatili wa kijinsia na kingono.”