Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Saidieni watoto wa Yemen watimize ndoto zao- Unicef

Akiwa nchini Yemen, Mkurugenzi Mtendaji wa Unicef, Henrietta H. Fore (pichani) alikutana na watoto kwenye kituo rafiki cha watoto kilichopo kwenye kituo cha afya cha  Alqatee'a kinachoendeshwa na UNICEF mjini Aden.
UNICEF
Akiwa nchini Yemen, Mkurugenzi Mtendaji wa Unicef, Henrietta H. Fore (pichani) alikutana na watoto kwenye kituo rafiki cha watoto kilichopo kwenye kituo cha afya cha Alqatee'a kinachoendeshwa na UNICEF mjini Aden.

Saidieni watoto wa Yemen watimize ndoto zao- Unicef

Msaada wa Kibinadamu

Miaka mitatu ya mapigano nchini Yemen imezidi kupeperusha ndoto za watoto wa nchi hiyo pamoja na kusigina haki zao za msingi, amesema Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF Henrieta H. Fore baada ya ziara ya siku nne nchini humo. 

Katikati ya mji wa Aden, nchini Yemen, msafara wa magari ukiwa na ugeni kutoka UNICEF akiwemo Mkugurenzi Mtendaji Bi. Henrietta H. Fore.

Mwelekeo ni kituo cha afya cha Alqatee’a ambako analakiwa na wauguzi na mama ambao watoto wao wamelazwa kupata huduma kutokana na magonjwa yanayokabili watoto wao ikiwemo utapiamlo uliokithiri.

Watoto hawa ni miongoni mwa watoto milioni 11 nchini Yemen ambao wanahitaji chakula, tiba, elimu , maji na huduma za kujisafi ambapo Bi. Fore amesema..

(Sauti ya Henrietta H. Fore)

“Tumekutana na akina mama kadhaa wakiwa na watoto wao, wengi wao ni wachanga, na mama hao wanahitaji msaada mbalimbali, kabla na baada ya kujifungua, ikiwemo lishe na malezi kwa watoto wao nyumbani.”

Ametembelea pia kituo cha watoto kinachofadhiliwa na UNICEF ambako watoto wanajifunza ikiwemo kuchora kama njia mojawapo ya kujieleza, na ndipo akaelezea moja ya mchoro aliopatiwa.

(Sauti ya Henrietta H. Fore)

“Anaonyesha dunia ambayo angependa awepo. Kuna basi limebeba abiria, kuna lori na pia taa za barabarani ambazo hazipo Aden, ameziona tu kwenye vitabu.Hapa anaonekana amependeza na rafiki yake wameketi. Kuna jua linawaka na nyumba anayopenda.”

Kwa mantiki hiyo ametoa wito kwa jamii ya kimataifa, Umoja wa Mataifa kuongeza usaidizi wao kwa Yemen ili watoto hao waweze kutimiza ndoto zao baada ya machungu waliyopitia na kushuhudia nchini mwao.