Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watu CAR wanakata tamaa kutokana na hali ya usalama- UN

Mlinda amani akiwa doria katika mtaa wa PK5 Bangui, Jamhuri ya Afrika ya Kati,CAR.
MINUSCA Photo
Mlinda amani akiwa doria katika mtaa wa PK5 Bangui, Jamhuri ya Afrika ya Kati,CAR.

Watu CAR wanakata tamaa kutokana na hali ya usalama- UN

Amani na Usalama

Watu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, wanateseka zaidi kutokana na hali ya usalama kuendelea kuvurugikahuku wakikatishwa tamaa na wale ambao wanapaswa kuwalinda.

Mtaalam huru wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa kwa CAR, Marie Thérèse Keita Bocoum amesema hayomjini Bangui, CAR hii leo baada ya kukamilisha ziara ya kikazi ya siku 10 katika nchi hiyo.

Kutokana na aliyoshuhudia, kuharibika kwa hali ya haki za binadamu nchini humo, Bibi Bocoum ameomba kuwepo kwa uratibu mzuri wa  juhudi za amani, sheria na kusameheana nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati.

 

Ahmad Al Gohary, askari wa kulinda amani  wa kikosi cha UN cha kulinda amani CAR- MINUSCA akifanya doria.
MINUSCA/Igor Rugwiza
Ahmad Al Gohary, askari wa kulinda amani wa kikosi cha UN cha kulinda amani CAR- MINUSCA akifanya doria.

Mtaalam huyo amesema, japo serikali inajitahidi kulinda watu wake, bado ina udhibiti  mdogo kwenye maeneo yote ya nchi hiyo huku makundi yenye silaha yaliyoko sehemu mbalimbali nchini humo yakiendeleza  ukatili.

Ameeleza wasiwasi wake kuhusu hali ya kutokuwepo kwa mawasiliano na uwazi baina ya washika dau wanaofanya kazi nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati akisema, “nasikitishwa na kuzorota kwa hali ya kibinadamu na kuongezeka kwa hali ya kutokuwa na usalama kufuatia operesheni za kijeshi mwezi Aprili pamoja na matukio ya Bangui mapema mwezi Mei ambapo raia kadhaa walipoteza maisha yao na pia nafasi za kuabudia kushambuliwa.”

Ameomba kuchukuliwa hatua za haraka kuunga mkono huduma za mahakama na pia kurejesha imani ya haki ya ukweli, vyenye lengo la kuzuia kutorudiwa tena kwa migogoro.

 

Mtaalam huru wa Umoja wa Mataifa wa masuala ya haki za binadamu kwa CAR,Marie Thérèse Keita Bocoum .
UN Photo - Jean-Marc Ferre
Mtaalam huru wa Umoja wa Mataifa wa masuala ya haki za binadamu kwa CAR,Marie Thérèse Keita Bocoum .

Pia Bi. Bocoum, ameshtushwa  na ongezeko la visa vya mashambulizi dhidi ya wafanyakazi wa mashirika yanayotoa misaada ya kibinadamu pamoja na vifaa vyao na kuwahimiza  maafisa wa maeneo hayo kuimarisha utawala wao na pia kulaani vitendo  vibaya.

Bi Bocoum atawasilisha rasmi  ripoti yake katika Baraza la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa mjini Geneva, Uswisi tarehe 4 mwezi ujao.