Taarifa za wahamiaji kutelekezwa jangwani zinasikitisha: IOM
Si haki kwa wahamiaji ambao ni pamoja na kina mama wajawazito na watoto kutelekezwa peke yao bila chakula wala maji au kutarajiwa wataweza kutembea kwa miguu maili kadha katika joto kali wakitafuta usalama jangwani.
Kauli hiyo ya masikitiko imetolewa na mkurugenzi mtendaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la wahamiaji-IOM, William Lacy Swing, alipogusia taarifa za wahamiaji waliokwama katika eneo la mpaka kati ya Algeria na Niger.
Kwa mujibu wa Leonrad Doyle msemaji wa IOM akiwa mjini Geneva Usiwisi, IOM inasikitishwa na hatima ya mamia ya wahamiaji ambao hujikuta wako njia panda na kuachwa wajitafutie chakula na malazi mpakani mwa Algeria na Niger. Ameongeza kuwa
“Uhamiaji unaodhibitiwa ndiyo suluhu pekee na wahamiaji wote wanapaswa kutendewa haki na kupewa fursa ya kuishi katika mazingira salama na yenye mpangilio.”
Amesema huo ndio wito wao kwa mataifa yote duniani. IOM inasema idadi ya wahamiaji wanaotembea kwa miguu kupitia jangwa kutoka Algeria hadi Niger imeongezeka kwani Mei 2017 wahamiaji 135 walitelekezwa mpakani na sasa imeongezeka hadi 2,888 April mwaka huu.
IOM inakadiria kuwa takriban wahamiaji 11, 276, wanawake na watoto, walivuka mpaka baina ya nchi hizo mbili mwaka huu.