Walinda amani wa MINUSMA watunzwa medali za UN
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, ametumia siku yake nzima leo na walinda amani wa ujumbe wa umoja huo mjini Bamako nchini Mali, MINUSMA ambapo amewatunza medali walinda amani wawili wa ujumbe huo.
Kabla ya kuvisha medali hizo, Katibu Mkuu alishiriki tukio maalum la kumbukizi ya walinda amani kwenye kambi ya MINUSMA kwa kuweka shada la maua katika mnara wa ujumbe huo ulio na majina ya walinda amani waliouawa wakiwa kazini.
MINUSMA ni operesheni inayoongoza kwa kushambuliwa mara kwa mara na mwaka jana pekee walinda amani 21 waliuawa pamoja na raia 7.
Guterres amesema,
walinda amani wamedhihirisha ujasiri wao
walinda amani, mmedhihirisha kuwa mnaweza kujitolea kwa dhati
hata kwa niaba ya wenzenu wengi, jambo ambalo ndilo kilele cha kujitolea kulinda maisha ya raia wa Mali. Nataka kuwapongeza kwa hilo na kujitolea kwenu na kusema najivunia kufanya kazi nanyi.”
Katibu Mkuu amesema walinda amani ndio alama ya Umoja wa Mataifa.
Waliovishwa medali ni Olufunmilayo Ajibike Amodu, kutoka Nigeria ambaye ametambuliwa kuwa afisa bora pamoja na Meja Mohammed Badrul Ahsan Khan, kutoka Bangladesh.
Bw Guterres anaandamana na Mkuu wa operesheni za ulinzi wa amani wa Umoja wa Mataifa Jean-Pierre Lacroix, Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF Henrietta H. Fore na Atul Khare ambaye ni msaidizi wa Katibu Mkuu kwenye operesheni za amani mashinani.
Awali Katibu Mkuu alilakiwa kwenye uwanja wa ndege na Rais Ibrahim Boubacar Keita wa Mali ambapo watakuwa na mazungumzo baadaye leo.
Kesho Jumatano Bwana Guterres anatarajiwa kutembelea maeneo ya mikoani nchini Mali ili kukutana na viongozi wa mamlaka mbalimbali, wakiwemo wawakilishi wa wanawake, vijana na viongozi wa kidini pamoja na wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa.