Hali ya kibinadamu si shwari Yemen : OCHA
Hali ya kibinadamu nchini Yemen inazidi kuzorota kutokana kuongezeka kwa migogoro, vikwazo dhidi ya misaada ya kibinadamu na kupungua kwa uingizaji wa biashara muhimu hivyo kusababishwa mamilioni ya waYemen kukabiliwa uhaba mkubwa wa chakula.
Mark Lowcock ambaye ni mkuu wa ofisi ya uratibu wa misaada ya kibinadamu na dharura ya Umoja wa Mataifa, OCHA amesema hayo kupitia taarifa yake iliyotolewa jijini New York, Marekani.
Bwana Lowcock amesema, zaidi ya watu milioni 22 nchini Yemen wanahitaji usaidizi wa kibinadamu ambapo milioni 8.4 kati yaohawana uhakika wa chakula.
Ameongeza kuwa katika sekta ya elimu, mtoto mmoja kati ya wanne hayupo shuleni kitu ambacho ni hatari kwa maendeleo ya baadaye katika soko la ajira.
Na huko kaskazini mwa Yemen, watumishi wa umma, ikiwa ni pamoja na walimu na wahudumu wa afya hawajapata mishahara yao kwa muda mrefu .
Ameseam usalama wa raia nchini Yemen upo hatarini kutokana na tatizo la makombora kurushwa kila uchao na kusababisha idadi kubwa ya vifo vya raia.
Tangu Desemba 2017, migogoro imeongezeka Taizz na sehemu ya pwani ya magharibi na zaidi ya watu 130,000 wamehama hivyo kufanya idadi ya kamili ya waliokimbia makazi yao kufikia milioni 3 tangu mwaka 2015.
Kufuatia hali hiyo ya wasiwasi mashirika ya kibinadamu yanazidi kukabiliwa na vikwazo vilivyowekwa na mamlaka katika maeneo ya kaskazini huku wafanyakazi wa mashirika ya kibinadamu wakifungwa na kutishiwa na visa zao ni kucheleweshwa au kukataliwa.
Aidha mkuu huyo wa OCHA amesema ametiwa moyo na majadiliano ya hivi karibuni yaliyofanyika kati kwa lengo la kupatia suluhu upitishaji wa mizigo kupitia bandari za Houdaydah na Saleef.
Halikdhalika OCHA inatoa wito kwa Serikali ya Yemeni, kuchukua hatua za kuimarisha uingizaji wa kibiashara, chakula, mafuta na misaada ya kibinadamu kupitia kila bandari hio za Yemen.
Pia imeitaka serikali ya Yemen kuchukua hatua ili kuhakikisha kuwa watumishi wote wa umma wanapata mishahara yao popote walipo Yemen.