Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Pande kinzani Sudan Kusini, maneno pekee hayatoshi- IGAD

Wakimbizi wa ndani katika kambi ya Lokoloko nchini Sudan kusini. Picha: UNMISS

Pande kinzani Sudan Kusini, maneno pekee hayatoshi- IGAD

Amani na Usalama

Baada ya pande kinzani nchini Sudan Kusini kuridhia sitisho la mapigano, IGAD imezitaka kusimamia ahadi hiyo ili hatimaye kuwepo na amani ya kudumu nchini humo.

Wito kwa pande hizo kinzani umetolewa na Mwenyekiti wa IGAD, ambayo ni mamlaka ya ushirikiano wa kibiashara wa nchi 8 za pembe ya Afrika, Afrika Mashariki na Maziwa Makuu. 

Workneh Gebeyehu ambaye ni mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri la nchi za IGAD akizungumza mwishoni mwa mkutano huo Addis Ababa, Ethiopia amesema, “Mambo yasiyozuilika lazima yatokee ambapo pande husika Sudan Kusini lazima zilegeze misimamo yao na kupitisha maamuzi ya kiuhalisia kwa ajili ya Amani Sudan Kusini. Ni kwa muktadha huo IGAD imewasilisha pendekezo kwa Imani kuwa litawasaidia kufikia makubaliano.” 

“Mambo yasiyozuilika lazima yatokee ambapo pande husika Sudan Kusini lazima zilegeze misimamo yao na kupitisha maamuzi ya kiuhalisia kwa ajili ya Amani Sudan Kusini. Ni kwa muktadha huo IGAD imewasilisha pendekezo kwa Imani kuwa litawasaidia kufikia makubaliano.”

Pendekezo hilo la IGAD linataka pande ya serikali na pande kinzani Sudan Kusini ziondoe pengo la misimamo yao kwenye masuala ya utawala na ulinzi, mambo ambayo pande hizo hazikuafikiana wakati wa mazungumzo yaliyoratibiwa na kanisa. “Baraza la IGAD linaamini kwa dhati kuwa pendekezo hilo lina mizania na limezingatia hali ya sasa ya kisiasa, kiuchumi na kijamii.”

Ingawa mkutano huo wa ngazi ya juu umemalizika huko Ethiopia bila makubaliano thabiti, angalau wameweka ahadi ya kimsingi ya kusitisha mapigano na kutekeleza ahadi ya kutenga asilimia 35 ya viti vya wanawake katika nafasi za uongozi kwenye ngazi zote za serikali.