Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Vyombo huru vya habari ni msingi wa utawala bora- UN

Waandishi wa habari.(Picha:UM/Isaac Billy)

Vyombo huru vya habari ni msingi wa utawala bora- UN

Sheria na Kuzuia Uhalifu

Umoja wa Mataifa umetaka serikali kuzingatia uhuru wa vyombo vya habari kwa kuwa ndio msingi wa utawala bora na serikali zinazowajibika kwa umma.

Katika ujumbe wake wa siku ya uhuru wa vyombo vya habari hii leo, Katibu Mkuu Antonio Guterres amesema vyombo hivyo vinasaidia kujenga uwazi na jamii za kidemokrasia pamoja na kuwajibisha walio madarakani.

Kama hiyo haitoshi amesema wanahabari wanaandika habari zinazopaswa kuandikwa ili kuinua ufahamu wa umma kuhusu mambo yanayowahusu.

Image
UNESCO limesisitiza usalama wa waandishi wa habari. Picha: UNESCO

Hata hivyo amesema..

(Sauti ya Antonio Guterres)

“Sheria zinazolinda uandishi huru wa habari, uhuru wa kujieleza na uhuru wa kupata habari lazima zipitishwe, zitekelezwe na zisimamiwe. Uhalifu dhidi ya wanahabari ushtakiwe.”

Wakati huo huo wataalamu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa wamestaajabishwa na kasi ya kutikiswa kwa uhuru wa vyombo vya habari hali ambayo wamesema inaweka mashakani jukumu la vyombo hivyo kushirikisha umma katika kuwajibisha serikali.

Image
Msikilizaji wa radio ya Kangema RANET nchini Kenya.(Picha:WMO/Video capture)

Mmoja wao, David Kaye amesema waandishi wa habari wanashambuliwa, uhuru wa kujieleza unabinywa na hata watu wanaofanya kazi na serikali hawapeleki matangazo ya biashara kwa vyombo vya habari vinavyokosa serikali iliyo madarakani.

Wamesema vyombo huru vya habari na vinavyojitegemea vinafanikisha demokrasia na uwajibikaji ilihali mashambulizi dhidi ya wanahabari na tasnia ya habari hukandamiza hoja ya ushiriki wa umma na uwajibishaji wa serikali.