Nchi zaidi ya 190 zasherehekea siku ya kimataifa ya Jazz:
Leo ni siku ya kimataifa ya muziki wa Jazz, na maadhimisho ya kimataifa mwaka huu yanafanyika St. Petersburg, Urusi.
Shirika la Umoja wa Mataifa la elimu , sayansi na utamaduni UNESCO linasema wasanii zaidi ya 30 wamekusanyika St. Petersburg kusherehekea siku hiyo kwa kutoa burudani katika tamasha maalumu akiwemo Luciana Souza kutoka Brazil.
UNESCO inaamini kwamba siku ya kimataifa ya jazz inaimarisha mawasiliano na utangamano katika jamii na lengo lake ni kuchagiza uhuru, ubunifu, majadiliano na kuunganisha watu kutoka kila kona duniani.
Maadhimisho ya leo mjini St. Petersburg Urusi yanaambatana na tamasha kubwa kwenye ukumbi wa kihistoria wa Mariinsky.
Wasanii wanaoshiriki wanatoka katika nchi 14.
Balozi mwema wa UNESCO, Herbie Hancock ambaye pia ni mpiga kinanda wa Kimarekani ndiye anayeongoza tamasha hilo linalojumuisha pia wasanii wengine maarufu kama Igor Butman wa Urusi, Cyrille Aimee wa Ufaransa na Till Brönner wa Ujerumani.
Akizungumzia umuhimu wa Jazz, Hancock anasema..
(Sauti ya Herbie Hancock)
“Jazz haina mipaka wala ukomo. Ni lugha ya dunia nzima ya usawa na amani.”
Mji wa st Petersburg unachukuliwa kama ni mji mkuu wa utamaduni wa Urusi na kupitia mji huo ndio muziki wa Jazz uliingia Urusi
UNESCO inasema lengo ni kuzileta pamoja jamii, shule, wasaniii, wanahistoria, wanazuoni na mashabiki kutoka kote duniani kujifunza kuhusu chimbuko la Jazz na ushawishi wake.
Kwa shirika hilo linaamini kwamba siku hii inazidi kuongeza uelewa kwamba mazungumzo ya tamaduni mbalimbali na uelewa ni lazima na yanadumisha ushirikiano na mawasiliano.