Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Zeid yuko ziarani Ethiopia atashiriki pia mkutano wa AU

Picha: UN/Jean-Marc Ferré
Kamishina Mkuu wa Haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Zeid Ra’aad al-Hussein.

Zeid yuko ziarani Ethiopia atashiriki pia mkutano wa AU

Haki za binadamu

Kamishina mkuu wa wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Zeid Ra’ad Al Hussein amewasili Ethiopia kwa ziara ya siku nne ambapo atakutana na maafisa wa serikali lakini pia kushiriki mkutano wa ngazi ya juu wa Muungano wa Afrika AU na Umoja wa Mataifa.

Akifafanua sababu za kuwa ziarani nchini humo baada ya kuwasili mjini Adis Abba  Zeid amesema

(SAUTI YA ZEID RA’AD AL HUSSEIN)

“Mosi ni kuzuru jimbo la Oromiya, tulisema tunataka kupata fursa ya kufika Ahmara na Oromiya na mamlaka ya Ethiopia imeturuhusu, ili ni ombi tulilolitoa nilipozuru hapa mara ya kwanza.”

Jimbo la Oromiya lililopo mpakani na Somalia limeshuhudia machafuko hivi karibuni yalioyowatawanya watu takriban milioni moja. Zeid amesema sababu nyingine ni

(SAUTI YA ZEID RA’AD AL HUSSEIN)

“Pili kukutana na waziri mkuu mpya Ahmed, ambaye aliteuliwa hivi karibuni na ambaye ametoa hotuba muhimu sana kuhusu utekelezaji wa haki za binadamu na tunataka kufuatilia kuhusu ahadi hizo.”

Ameongeza kuwa wadau  wa Muungano wa Afrika AU ni muhimu katika kufanikisha ajenda hiyo

(SAUTI YA ZEID RA’AD AL HUSSEIN)

“Tatu ni kukutana na uongozi wa Muungano wa Afrika kujadili jinsi gani tutaunda mkakati pamoja nao kwa namna ambayo uhisiano wao na Umoja wa Mataifa utakuwa katika nguzo muhimu tatu zikijumuisha haki za binadamu.”

Zeid pia atatoa hotuba ya ufunguzi wa mkutano wa ngazi ya juu wa AU na Umoja wa Mataifa kuhusu haki za binadamu kabla ya kuhitimisha ziara yake ya pili nchini Ethiopia.