Ofisi ya haki za binadamu yalaani mauaji ya waandamanaji Gaza
Ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa imelaani matumizi yasiyo ya lazima ya silaha za moto yaliyofanywa na vikosi vya usalama vya Israel dhidi ya waandamanaji wa kipalestina kwenye mpaka wa Gaza na Israel
Ofisi hiyo kwa ushirikiano na jopo huru la wataalamu wa haki za binadamu, na mahakama ya kimataifa , wametoa wito wa kusitisha mgogoro huo na kutaka uchunguzi kufanyika mara moja ili kubaini wahusika wa mauajiyaliotokea hivi karibuni dhidi ya raia 28 wa kipalestina na wengine 1600 walijeruhiwa.
Mmoja wa wataalam wa Umoja wa Mataifa amesema ijapokuwa ahadi ya Israel ya kufanya uchunguzi wa mauaji hayo, bado haijatekelezwa, vikosi vyao vya usalama vinaendelea kutumia silaha za moto, ambazo zinaendelea kuwaua na kuwajeruhi waandamanaji wa kipalestina ikiwemo wanawake na watoto.
Pia amesema visa vya majeruhi na mauaji yaliyotokea tangu mwanzoni mwa maandamano hayo tarehe 30 mwezi uliopita na vikosi vya usalama vya Israel, vimekiuka mkataba wa kimataifa wa haki za kibinadamu wa mwaka 1966, na matumizi yasio ya lazima ya silaha za moto ya vikosi vya usalama ya mwaka 1990, chini ya azimio la Geneva la mwaka 1949 lamatumizi ya nguvu dhidi ya waandamanji.