Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watendeeni wema wahamiaji Yemen- UNHCR

Wahamiaji hawa wakihesabiwa kabla ya kusafirisha kwa boti kutoka Obock, kaskazini mwa Djibouti kuelekea Yemen. Licha ya mzozo Yemen bado watu wanamiminika kusaka hifadhi.
Kristy Siegfried/IRIN
Wahamiaji hawa wakihesabiwa kabla ya kusafirisha kwa boti kutoka Obock, kaskazini mwa Djibouti kuelekea Yemen. Licha ya mzozo Yemen bado watu wanamiminika kusaka hifadhi.

Watendeeni wema wahamiaji Yemen- UNHCR

Wahamiaji na Wakimbizi

Umoja wa Mataifa una wasiwasi mkubwa juu ya madhila yanayokumba wahamiaji, wasaka hifadhi na wakimbizi wapya nchini Yemen. Yaelezwa manusura  hufyatuliwa risasi, hupigwa kila mara, hubakwa na hata huvuliwa nguo na kusalia uchi.

 

Wahamiaji, wakimbizi na wasaka hifadhi wapya wanaoingia wengi  nchini Yemen kwa sasa wanakabiliwa na magumu kutokana na mgogoro unaoendelea huko ambao unasababisha mateso ya aina mbalimbali  hasa kwa wageni wapya wanaowasili huko. Taarifa kamili na Assumpta Massoi.

Msemaji wa wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR, William Spindler, amesema hayo leo akizungumza na waandishi habari mjini Geneva Uswisi.

Amesema wanaguswa na hali  inayoendelea  kuharibika hususan kwa wahamiaji, wakimbizi na wasaka hifadhi wapya nchini Yemen.

(Sauti ya William Spindler)

“Taarifa za unyanyasaji ndani mwa vituo vya kuwazuialia ni nyingi ambapo baadhi ya wageni wapya hunyanyaswa kingono. Manusura  wameielezea UNHCR visa vya kufyatuliwa risasi, kupigwa kila mara, ubakaji wa watu wazima na watoto pamoja na udhalilishaji kama vile kuwavua nguo na kubaki uchi. Wakati mwingine hulazimishwa kushuhudia mauaji ya wenzao na pia kunyimwa chakula.”

Spindler amesema mgogoro unaoendelea nchini humo pamoja na hali ya kutokuwepo na usalama  hutishia taasisi za dola na pia kudhoofisha utawala wa  wa sheria.

Amesema hali hiyo imesababisha kuongezeka kwa visa vya kuwasafirisha kiharamu binadamu,kuwafukuza kutoka nchini humo na pia kudai pesa kutoka kwa wahamiaji. Ametaka wahusika kuwatendea mema wahamiaji.

Msemaji ameongeza kuwa  kuanzia Februari  mwaka huu, UNHCR imekuwa ikishughulikia  hali ambapo wageni takriban 100 waliofika Yemen  waliweza kukamatwa na kuwekwa ndani.

Walio kamatwa wanasema kuwa  hutishiwa kurejeshwa walikotoka kwa nguvu pamoja na kunyanganywa mali zao na wanaowalangua au wakiwa vizuizini.