Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watu zaidi ya 250 wapoteza maisha kwenye ajali ya ndege Algeria

Katibu Mkuu wa UM Antonio Guterres
PICHA/UN/Evan Schneider(maktaba)
Katibu Mkuu wa UM Antonio Guterres

Watu zaidi ya 250 wapoteza maisha kwenye ajali ya ndege Algeria

Masuala ya UM

Abiria zaidi ya 250 na wahudumu wa ndege wamepoteza maisha leo asubuhi katika ajali mbaya iliyohusisha ndege ya kijeshi nchini Algeria. 

Katika tarifa iliyotolewa na msemaji wake Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema amepokea kwa masikitiko makubwa tarifa za ajali hiyo iliyotokea karibu na mji mkuu Algiers.

Duru za habari zinasema ndege hiyo ilianguka muda mfupi baada ya kupaa kutoka uwanja wa ndege wa kijeshi wa Boufariki Magharibi mwa Algiers.

Jumla ya watu 257 wamefariki dunia wengi wakiwa ni wanajeshi na familia zao wakijumuisha wanawake na watoto, pia wahudumu wa ndege 10, raia wa Sahara Magharibi 30 na wajumbe 26 wa Polisario ni miongoni mwa waliokufa.

Katibu Mkuu ametuma salamu za rambirambi kwa familia za waliopoteza maisha, watu na serikali ya Algeria kufuatia msiba huo mkubwa. Nayo serikali ya Algeria imesema uchunguzi unafanyika ili kubaini chanzo cha ajali hiyo ambayo ni mbaya zaidi kuwahi kutokea nchini humo.