Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Messi kupeperusha bendera ya utalii

UNWTO inasisitiza utalii unaojali tamaduni ya jamii husika, ununuzi wa bidhaa za eneo husika na pia kulinda urithi wa eneo husika. Huo ndio utalii unaowajibika kwa jamii.
Picha/WTO
UNWTO inasisitiza utalii unaojali tamaduni ya jamii husika, ununuzi wa bidhaa za eneo husika na pia kulinda urithi wa eneo husika. Huo ndio utalii unaowajibika kwa jamii.

Messi kupeperusha bendera ya utalii

Masuala ya UM

Wacheza soka nao wana nafasi yao kuchagiza utalii unaojali siyo tu mazingira bali pia jamii na ndio hapo Lionel Messi anajumuika!

Lionel Messi, mwanasoka nguli wa kimataifa kutoka Argentina ameteuliwa kuwa balozi wa shirika la utalii la Umoja wa Mataifa, UNWTO akijikita katika kuchagiza utalii unaowajibika kwa jamii.

Messi ametangazwa hii leo huko Madrid, Hispania ambapo amesema ni fursa ya kipekee na atatumia fursa hiyo kuhakikisha utalii unawajibika kwa jamii.

Amesema wakati wa safari zake ikiwemo za kitalii amepata fursa ya kufahamu tamaduni nyingine na kutambua ni jinsi gani tamaduni hizo zinafanya ulimwengu huu kuwa wa kipekee na hivyo amefurahi kujiunga na shirika hilo katika kuchagiza utalii bora.

Katibu Mkuu wa UNWTO Zurab Pololikashvili amesema Messi ni mwanasoka wa kipekee na mfano wa jinsi kujituma kwa dhati kunaweza kuleta matokeo bora.

Amesema shirika lake linajivunia kuwa na Messi kama mmoja wa mabalozi wake wa kusongesha maadili bora na manufaa mazuri yanayoletwa na utalii.

Messi ni mwanasoka wa kwanza duniani kushinda tuzo tano za kiatu cha dhahabu ambapo kati tuzo hizo tano, nne alishinda mfululizo.