Hongera askari wetu kwa kuwazuia magaidi wa Al-Shabaab-AMISOM
Walinda amani wanne wameuawa na wengine sita kujeruhiwa nchini Somalia mapema leo wakati askari wa kikosi cha kulinda amani cha muungano wa Afrika nchini Somalia -AMISOM- kilipokabiliana kijeshi na wapiganaji wa Al-Shabaab.
Taarifa iliyotolewa leo jumatatu na AMISOM imesema kuwa vikosi vyao vilifanikiwa kuwarudisha nyuma magaidi wa Al -Shabab baada ya kushambulia kambi tatu za vikosi vya AMISOM katika eneo la Lower Shabelle.
Taarifa imemnukuu mjumbe maalum wa mwenyekiti wa tume ya Muungano wa Afrika kuhusu Somalia, balozi Francisco Caetano Madeira, akisifu jeshi la Muungano wa Afrika katika eneo la Lower Shabelle kwa kuonyesha ujasiri wao wakipambana dhidi ya magaidi wa Al Shabaab.
Taarifa imeongeza kuwa Al Shabaab walihujumu mara kadhaa kambi za jeshi zilizoko Quoryole, Bulomareer na Golwein na washambuliaji walipata cha mtema kuni.Katika mapigano hayo Al Shabaab takriban 30 wameuawa na magari manane yaliyowabeba yaliharibiwa pamoja na magari mawili yaliyokuwa yamejazwa vilipuzi nayo yameharibiwa huku silaha kadhaa zikikamatwa.
Upande wa AMISOM ulipoteza askari wake wanne ilhali wengine sita wakijeruhiwa.